KLABU ya Yanga imefanikiwa kuingia fainali ya Kombe la Mapinduzi na kuwaondosha Azam FC kwa mikwaju ya penati 5-4, baada ya kutoshana nguvu kwenye dakika 90 za mchezo. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Nusu fainali hiyo ya kwanza ilipigwa kwenye Uwanja wa Amani, Zanzibar majira ya saa 10 jioni, huku nyingine ikichezwa baadae majira ya saa 2 usiku ambapo itawakutanisha Simba dhidi ya Namungo.
Yanga ndio walikuwa wa kwanza kupata bao kwenye mchezo huo kupitia kwa Tuisila Kisinda dakika ya 51, na baadae Obrey Chirwa alisawazisha bao hilo dakika ya 67 akiunganisha mpira uliopigwa na Bruce Kangwa mlinzi wa kushoto wa Azam FC.
Katika mchezo huo timu zote mbili zilionekana kucheza kwa taadhari huku kila mmoja ikiwa makini kwa kutompa mwenzie nafasi katika dakika zote za mchezo.
Kwa matokeo hayo Yanga itasubiri kuungana na mshindi wa mchezo kati ya Namungo na Simba kwenye nusu fainali ya pili itakayopigwa kwenye Uwanja huo huo wa Amani.
Finali hiyo inatachezwa siku ya Jumatano tarehe 13 Januari, 2021 majira ya saa 2 usiku kwenye Uwanja wa Amani visiwani Zanzibar.
Leave a comment