MBUNGE wa Kawe (CCM), Askofu Josephat Gwajima, ameishauri Serikali iitishe mdahalo wa wazi, ili kumaliza utata juu ya chanjo ya Ugonjwa wa Korona (UVIKO-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Askofu Gwajima ametoa wito huo leo Jumapili, tarehe 22 Agosti 2021, akihubiri katika Kanisa lake la Ufufuo na Uzima, lililopo Ubungo mkoani Dar es Salaam.
“Ningekuwa waziri wa afya ningesema hivi, Gwajima si unadai chanjo sio salama tufanye mdahalo, wewe Gwajima unayedai chanjo sio salama njoo utuelezee si salama kiasi gani? Na sisi tunaodai chanjo salama ni salama kiasi gani na uwe mjadala wa wazi Watanzia wote waone,” amesema Askofu Gwajima.
Askofu Gwajima ameongeza “ si tufanye hivyo, kwanza mimi nitaanza kwa kuchagua siku iwe Alhamisi hii, chagua siku kwamba yeye askofu kwa mujibu anasema si salama na sisi tunasema ni salama. Tukutane kwenye mdahalo wa wazi.”
Mbunge huyo wa CCM, amedai kwamba yeye ana watu wake ambao wanaunga mkono msimamo wake wa kukataa chanjo hiyo isitolewe kwa wananchi hadi Tanzania itakapofanya uchunguzi dhidi yake.
“Mimi nitakuja na kundi langu linalosema si salama na wewe utakuja na kundi lako linalosema ni salama. Tunajadili wote ili Watanzania wote waone,” amesema Askofu Gwajima.
“Kuwepo na mahala pa kutoa ripoti, sio kuwe na kijiji kizima umeshadunga, umeshaondoka. Hili mimi nasema hapana, tuwe na akili ya ziada kwenye kumsaidia rais. Nyie mawaziri muwe na akili ya kutimiza mission ya rais kwa kutumia inteljensia yenu,” amesema Askofu Gwajima na kuongeza:
“Kuwe na followup (ufuatiliaji) watu waliochanjwa wanaendeleaje, lakini hatujui tunasema wako laki mbili waliochanjwa lakini wanaendeleaje, is not an issue. Kwamba chanjo nzuri au mbaya.”
Rais Samia Suluhu Hassan, tarehe 28 Julai 2021 Ikulu ya Dar es Salaam, alizindua zoezi la utoaji chanjo ya Korona.
Akizundua chanjo hiyo, Rais Samia aliwatoa wasiwasi Watanzania kwamba chanjo hiyo iko salama kwa vitendo, baada ya kuchanjwa aina ya Johnson & Johnson.
Leave a comment