MBUNGE mteule wa Nkasi Kaskazini kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) nchini Tanzania, Aida KhenanIi amesema, kamwe hatowasaliti wananchi waliomchagua hivyo atakwenda Bunge kuapishwa ili aweze kuwatumikia. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Aida ni mgombea pekee wa Chadema aliyeibuka mshindi katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano ya tarehe 28 Oktoba 2020 akimwangusha Ally Kessy wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) aliyekuwa anatetea jimbo hilo ambalo aliliongoza kwa miaka kumi mfululizo.
Uchaguzi huo, ulishuhudia vigogo wa upinzani zaidi ya 40 wakiongozwa na aliyekuwa kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, Freeman Mbowe wakishindwa uchaguzi huo.
Jumamosi iliyopita ya tarehe 31 Oktoba 2020, vyama vya Chadema na ACT-Wazalendo kwa pamoja vilitangaza kutoyatambua matokeo ya uchaguzi yaliyosimamiwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) na Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC).
Viongozi wakuu wa vyama hivyo, Mwenyekiti wa CHadema, Freema Mbowe, Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad, Kiongozi wa chama hicho, Zitto Kabwe na aliyekuwa mgombea urais wa Tanzania kupitia Chadema, Tundu Lissu walitoa tamko la pamoja.
Miongoni mwa mambo waliyokubaliana kushirikiana na kuitisha maandamano ya amani yasiyokuwa na kikomo nchi nzima ni kutaka uitishwe upya uchaguzi pamoja na kutotambua matokeo hayo.
Hata hivyo, Aida aliyekuwa mbunge wa viti maalum katika Bunge lililopita akizungumza na wananchi wa Nkasi Kaskazini amesema, hawezi kuwasaliti wananchi waliomchagua na anachokisubiri kwa sasa ni kuapishwa.
“Chama kiliniamini kikarudisha mamlaka kwa wananchi na wananchi wamenipa mamlaka. Kama niliapa Chadema siwezi isaliti Chadema hali kadhalika siwezi wasaliti wananchi wa Nkasi Kaskazini.”
Leave a comment