Friday , 17 May 2024
Home Habari Mchanganyiko AICC, JNICC yajipanga kukusanya bilioni 120
Habari Mchanganyiko

AICC, JNICC yajipanga kukusanya bilioni 120

Spread the love

MKURUGENZI Mtendaji wa Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC), Ephraim Mafuru amesema malengo yao ya mwaka 2023/2024 ni kukusanya Sh 120 bilioni kwa mwaka. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)

Mafuru amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati akielezea majukumu ya taasisi hiyo mbele ya wahariri na waandishi wa habari, huku akiweka wazi kuwa lengo lao ni kushiriki kuchangia pato la taifa na uchumi kwa ujumla.

Amesema Sh 120 bilioni ambayo wanarajia kukusanya kwa mwaka ni kupitia AICC, Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere (JNICC), Hopitali ya AICC, ofisi na nyumba ambazo wamepangisha watu.

“Tumejipanga kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 120 kupitia mikutano 30 kwenye kumbi zetu za AICC na JNICC, hospitali yetu na nyumba, hili limetafanikiwa kwa kuwa Rais Samia Suluhu Hassan amekuwa kiongozi wa kutangaza fursa za mikutano hapa nchini, amesema.

Mkurugenzi huyo amesema kwa mwaka wa 2022/2023 wameweza kuandaa mikutano 18, hivyo kwa mipango ambayo wamejiwekea watahakikisha Tanzania inaongoza katika Bara la Afrika kuandaa mikutano, ambapo kwa mwaka wa fedha wa 2023/2024 wameshaandaa mikutano minne ya kimataifa.
“Mwaka huu wa fedha tumeandaa mkutano wa kimataifa wa Rasilimali Watu, Jukwaa la Mifumo ya Chakula Afrika (AFS-Forum), ICMDA na PCCB na tuna maombi mengine mengi natarajia tutafikia lengo la mikutano 30,” amesema.

Mafuru amesema kwa miaka ijayo matarajio ni kuandaa mikutano 50 ambayo itawezesha sekta hiyo kuchangia zaidi ya shilingi mbilioni 350 kwa mwaka, ikiwemo dola za Marekani ambazo zimekuwa adimu.

“Vituo vya mikutano ndo vinachangia kwa asilimia kubwa ikifuatiwa na hospitali, AICC imechangia zaidi ya Sh bilioni 5.4 na JINCC bilioni 4.4, hospitali bilioni 4.5 ambazo kwa sasa zimeanza kupanda na tunaamini tutazipandisha zaidi, ni kweli tumejiendesha kwa hasara kwa miaka kadhaa lakini kuanzia 2021/2022 tumeendelea kujiendesha kwa faida, mwaka 2022 tumejiandaa kwa faida kutoka kwenye hasara ya milioni 500 kwenda kwenye faida ya bilioni 1.1” ameeleza Mafuru.

Mkurugenzi huyo amesema wapo kwenye hatua za mwisho za kuanza ujenzi wa Kituo cha Kimataifa cha Mlima Kilimanjaro (MKICC) ambao utakuwa na sifa za kimataifa, ikiwemo kuhudumia watu wengi, hivyo wanaamini malengo yanaenda kufikiwa.

Mafuru amesema ili kufikia malengo wamejikea malengo na kwamba hatamvumilia mtu yoyote atakakwenda kinyume na makubaliano, hata kama ameletwa na mtu.

Mkurugenzi huyo amesema ukumbi wa AICC una uwezo wa kuhudumia watu 1,350 kwa wakati mmoja, pamoja na kumbi ndogo 17 ambazo zinaweza kuingiza watu 400 hadi 10.
“JNICC inaweza kubeba watu, 1,003 hadi 1,213 kwa wakati mmoja, kuna kumbi ndogo za kutosha, lakini pia una vifaa kisasa,” amesema.

Amesema miaka minne iliyopita Tanzania ilikuwa inashika nafasi ya 13 na kuchangia soko kwa asilimia 5 kwa Afrika, ila kwa sasa wanashika nafasi ya tano na kuwa na mchango wa asilimia 10 katika soko.

Mafuru ametaja nchi ambazo zipo mbele ya Tanzania ni Afrika Kusini, Morocco, Rwanda na Misri ambapo wamebaini sababu ya kushindwa, hivyo wamejipanga kukabiliana na washindani wao.

Amesema utalii wa mikutano una mchango mkubwa katika uchumi, kwa kuwa unahusisha mnyororo wa thamani kwa kundi kubwa ikiwemo watoa huduma za chakula, mapambo, mahema, hoteli, usafiri na wengine.

Mkurugenzi huyo amesema kwa upande wa Hospitali ya AICC yenye vitanda 32 na kuhudumia 90,000 kwa mwaka na inatoa huduma bora.

Mafuru amesema AICC na JNICC vitakuwa vituo vya mikutano ambavyo vitahakikisha mnyororo wa thamani unaoneka kwa wadau wote ambao wanahusika na huduma za mikutano.

Kwa upande mwingine Mafuru ameeleza kusikitishwa na baadhi ya taasisi za Serikali kushindwa kulipa fedha za kukodisha kumbi za mikutano za vituo hivyo na kwamba wanashindwa kuteleza mipango yao kwa ufanisi.

“Tunadai zaidi ya shilingi bilioni 7.4 kwa taasisi 20 ambapo 17 ni za Serikali, huku asilimia 65 ya madeni ambayo ni zaidi ya shilingi bilioni 3.2 yakiwa yana zaidi ya miezi sita, hii sio sawa wanatukwamisha, tunaomba watulipe, ili tuweze kutekeleza mipango yetu,” amesema.

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Udhibiti wa serikali wakera asasi za kiraia

Spread the loveBaadhi ya wadau wa demokrasia na viongozi wa asasi za...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Nape aomba bajeti ‘kiduchu’ kwa mwaka 2024/25

Spread the loveWaziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Seneta: Wanasiasa hawasaidii mchakato wa Katiba mpya

Spread the loveSeneta wa jimbo la Busia, nchini Kenya, Okiya Okoiti Andrew...

Habari Mchanganyiko

Wananchi washauriwa kuongeza uelewa wa kujikinga na majanga

Spread the love WITO umetolewa kwa wananchi kuongeza uelewa na utayari kabla...

error: Content is protected !!