JUMLA ya abiria 30, marubani wawili na mhudumu mmoja wamenusurika kifo katika ajali ya ndege iliyotokea leo saa 3:40 asubuhi katika Hifadhi ya Taifa Mikumi mkoani Morogoro. Anaripoti Mwandishi Wetu …(endelea).
Ndege hiyo ya kampuni ya Unity Air 5H-MJH aina ya EMBRAER 120 iliyokuwa ikitokea Zanzibar ilipata tatizo la kiufundi wakati ikitua katika kiwanja cha ndege cha Kikoboga kilichopo katika hifadhi hiyo ya Mikumi.
Taarifa iliyotolewa Afisa Uhifadhi Mwandamizi Kitengo cha Mawasiliano wa Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA), Catherine Mbena imesema juhudi kubwa zimefanywa na marubani wa ndege hiyo pamoja na maofisa katika kiwanja hicho kuhakikisha kuwa hakuna madhara yatakayotokea kutokana na ajali hiyo.
“Abiria wote 30, marubani wawili, pamoja na mhudumu wa ndege hiyo wako salama na wanaendelea na ratiba yao ya kufanya utalii hifadhini.
“Matumizi ya kiwanja pamoja na shughuli za utalii zinaendelea kama kawaida,” amesema na kuongeza kuwa;.
“TANAPA imefanya taratibu zote za kuwasiliana na idara ya uchunguzi wa ajali za ndege itiyopo Wizara ya Uchukuzi –(AAIB) kwa ajili ya taratibu zingine na uchunguzi zaidi juu ya tukio hili,” amesema.
Amesema shirika linatoa shukrani kwa kikosi cha zimamoto na uokoaji Mikumi kwa ufanisi mkubwa katika changamoto hii.
Leave a comment