UPANDE wa Serikali, umeiomba Mahakama Kuu, Masjala Kuu, jijini Dar es Salaam, kupata kibali cha kuwauliza maswali ya dodoso wajumbe wa Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kuhusu hati zao kinzani walizowasilisha katika kesi iliyofunguliwa na wabunge viti maalum 19. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ni katika kesi Na. 36/2022 iliyofunguliwa na wabunge hao wakiongozwa na Halima Mdee, dhidi ya Chadema, Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kupinga uamuzi wa chama hicho kuwafukuza kinyume cha Sheria.
Ombi hilo limewasilishwa leo tarehe 9 Machi 2023, na Wakili wa Serikali, Stanley Kalokola, mahakamani hapo mbele ya Jaji Cyprian Mkeha.
Akiwasilisha ombi hilo, Wakili Kalokola ameomba fursa hiyo akidai kwamba kwa mujibu wa sheria kama hawatapa nafasi hiyo, watakakosa fursa ya kuwahoji wajumbe hao ambao ndio mashahidi katika kesi.
Wakili Kalokola anadai kuwa, wanaomba kuwafanyia dodoso wajumbe hao wa Chadema kwa kuwa katika kiapo chao kinzani aya ya nane wametengeneza ushahidi unaoathiri maslahi ya mjibu maombi wa pili na wa tatu (AG na NEC), na kwamba haki pekee waliyokuwa nayo pindi watakapoathirika ni kuwadodosa mashahidi hao.
“Sababu sheria haielezi Nini kifanyike pale wajibu maombi wawili wanapoathirisna, ni wajibu wetu kumdodosa maana yake tusipofanya hivyo kila anachokisema ndiyo uhalisia, kwa minajili hiyo ni ombi letu wakati mashahidi walioapa kiapo kinzani pamoja wanadodoswa na waleta maombi, basi mjibu maombi wa pili na wa tatu wapewe fursa sawa kudodosa kwenye maeneo ambayo yamemuathiri,” amedai Wakili Kalokola.
Hata hivyo, kiongozi wa Jopo la Mawakili wa Chadema, Peter Kibatala, ameweka pingamizi dhidi ya ombi hilo wakiitaka mahakama ilitupilie mbali kwa madai kwamba liko kinyume cha sheria kwa kuwa limewasilishwa nje ya muda.
Wakili Kibatala alidai kuwa, wakati waleta maombi (kina Mdee), wanaomba nafasi ya kuwauliza maswali ya dodoso mashahidi hao, walipaswa kutumia fursa hiyo kuomba.
Ombi hilo la Serikali linajiri baada ya mawakili wa wabunge viti maalum, kupewa nafasi ya kuwahoji maswali ya dodoso wajumbe sita wa Bodi ya Wadhamini ya Chadema, akiwemo Dk. Azavel Lwaitama, Ruth Mollel, Mary Joackim, Francis Mushi, Maulidah Anna Komu na Ahmed Rashid Hamis.
Vigogo hao wa Chadema, waanza kuhojiwa Leo mahakamani hapo, huku Dk. Lwaitama akifungua dimba Hilo akifuatiwa na Mollel, ambapo watahojiwa na mawakili WA kina Mdee wakiongozwa na Ipilinga Panya.
Kesi hiyo inaendelea kusikilizwa ambapo Jaji Mkeha, anaendelea kusikiliza hoja za pande zote mbili kwa ajili ya kutoa uamuzi.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online.
Leave a comment