WAGOMBEA Ubunge Arusha Mjini, Mrisho Gambo wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Godbless Lema wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) wamekutana katika mgahawa wa Safari Bistro jijini humo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea)
Wawili hao ambao wamekuwa na mchuano mkali kuwani jimbo hilo katika Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020 wamekutana mgahawani hapo leo Jumanne 29 Septemba 2020.
Lema anatetea jimbo hilo ambalo ameliongoza kwa miaka kumi mfululizo huku Gambo aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha akijitosa kwa mara ya kwanza kutaka kurejesha jimbo hilo chini ya himaya ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Wanasiasa hao, wamepiga picha kadhaa wakiwa kwenye mgahawa huo na kila mmoja ameiweka kwenye kuraza zake za mitandao ya kijamii na kuiandikia maelezo ya kufarijiana kwa kile kitakachotokea baada ya uchaguzi mkuu.
“Leo tumekutana mbunge ninaeingia madarakani na mbunge aliyemaliza muda wake! Ameniambia kuwa hajawahi kuwa na uchaguzi mgumu kama mwaka huu na amejiandaa kisaikolojia.”
“CCM ni chama kubwa hatuwezi kukosa kazi ya kumpa. Hakika nyumbani kumenoga!,” ameandika Gambo
Wakati Gambo akiandika hivyo kwenye ukurasa wake wa Twitter, mshindani wake mkubwa Lema, ameweka picha Instagram na kuandika “nimekutana na huyu kijana hapa Safari Bistro cafe… akaomba picha, nikasema ni sawa tu, kwani akose Ubunge hata na picha na mimi wajameni…hali yake ni ya majonzi sana.”
Leave a comment