DAKTARI John Magufuli, mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amesema anataka kukaa Ikulu kwa miaka 10 kama Rais Mstaafu, Jakaya Kikwete ili akamilishe miradi aliyoanzisha. Anaripoti Mwandishi Wetu, Kishapu … (endelea).
Ametoa kauli hiyo leo tarehe 4 Septemba 2020, wakati akiomba kura wananchi wa Kishapu mkoani Shinyanga, akiwa njiani kuelekea Mara kuendelea na kampeni zake za urais.
Akizungumza na wananchi hao, Dk. Magufuli ameomba apewe tena miaka mitano ili aonyeshe dunia itakavyokwenda.
“Amekuja Mzee Kikwete mmepima kwa miaka 10, mimi miaka mitano ndio maana nawaomba mnipe tena miaka mitano, tuone dunia itakavyokwenda,” amesema Dk. Magufuli.
Amesema, katika kipindi cha miaka mitano ya uongozi wake, ameleta maendeleo licha ya kwamba baadhi ya watu wanabeza utendaji wake.
“Tunaingia awamu ya pili ya uchumi, hakuna alietegemea pale Maswa kuwe na viwanda vya chaki, hapa Muwena barabara ya lami nzuri na wanapita watu wa vyama vyote.
“Hata wanaotukana wanapita hapa hapa, shukrani ya punda ni mateke lakini sisi wajibu wetu nikufanya kazi kwa ajili ya Watanzania wote,” amesema Rais Magufuli.
Dk. Magufuli amewaomba wana CCM na Watanzania kwa ujumla kumchagua kwa kuwa, maendeleo hayana chama.
“Ndio maana nawaomba wana CCM wenzangu na wa vyama vingine mtupe kura, sababu maendeleo hayana chama,” amesema.
Leave a comment