JOHN Mnyika, Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ameeleza kukerwa na kauli kwamba ‘wapinzani waongo, matapeli.’ Anaripoti Mwandishi Wetu, Tabora…(endelea).
Ni baada ya kueleza kwamba, vyama vya upinzani vimeshambuliwa na Dk. John Magufuli, mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), akiwaita waongo na matapeli.
Akizungumza katika mkutano wa kampeni za urais za Chadema jana tarehe 3 Septemba 2020, mkoani Tabora Mnyika amedai, wagombea wa chama chake ngazi ya urais sio waongo wala matapeli.
“Rais Magufuli, mgombea wa CCM jana (juzi) alikuwa Mkoa wa Tabora, katika baadhi ya wilaya za mkoa wenu na mgomeba huyu wa CCM, anawaambia Watanzania eti wasichague wagombea urais ambao yeye amewaita waongo, matapeli wanatoa ahadi za uongo,” amesema Mnyika.
Mnyika amehoji “nimesimama kuwakumbusha uongo wa Magufuli na CCM katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 walisema uongo kwa maneno na kwenye ilani yao kwamba, kipindi cha miaka mitano watatoa mil. 50 kwa kila kijiji, muongo ni nani?”

Mnyika amesema, Rais Magufuli ameshindwa kutekeleza ahadi yake ya kutoa Kompyuta Mpakato (Lapotop) kwa walimu, ajira kwa vijana pamoja na kuboresha masilahi ya watumishi wa umma.
“Rais Magufuli huyu, mgombea wa CCM aliahidi kutoa laptop kwa walimu uongo mtupu, mgombea huyu wa CCM mwaka 2015 aliahidi ajira badala ya kuleta ajira kwa Watanzania amepunguza ajira.
“Aliahidi katika kipindi cha miaka mitano wataboresha masilahi ya watumishi wa umma, lakini uongo mtupu hakuna nyongeza,” amesema Mnyika.
Katibu Mkuu huyo wa Chadema amesema, CCM imeshindwa kutekelezaahadi yake ya kuendeleza mchakato wa Katiba Mpya, na kwamba endapo Tundu Lissu, mgombea urais kupitia chamha hicho atachaguliwa kuwa rais, Serikali ya Chadema itaendeleza mchakato huo, ndani ya siku 100 tangu kuingia Ikulu.
“Nihitimishe kwa ahadi moja ambayo ilikuwa kwenye kitabu cha Ilani ya CCM kwenye Uchaguzi Mkuu 2015, iliwaahidi Watanzania na Rais Magufuli alizunguka kila mahali kuwa ahidi kwamba akichaguliwa CCM itaendeleza mchakato wa Katiba Mpya.
“Alivyoingia madarakani akaikana kwamba, CCM haikuwahi kuahidi mchakato wa katiba mpya,” amesema Mnyika.
Mnyika amewaomba wananchi wa Tabora na Tanzania kwa ujumla kumchagua Lissu na Salum Mwalimu, Mgombea wake mwenza ili awaondolee changamoto zao.
“Kwa uongo huu peke yake wa CCM, tunakila sababu ya kuwaadhibu tarehe 28 Oktoba kwa kumchagua Lissu kuwa rais, tuna kila sababu tarehe 28 Oktoba kumpunzisha Magufuli na kuipunzisha CCM,” amesema Mnyika.
Leave a comment