KESI ya uchochezi inayomkabili Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini imekwama baada ya kiongozi huyo mkuu wa Chama cha ACT-Wazalendo na wadhamini wake kutohudhuria. Anaripoti Faki Sosi…(endelea).
Kutokana na kutofika kwao, mahakama imeagiza Zitto na wadhamini wake kufika mahakamani hapo kujieleza sababu za leo tarehe 11 Machi 2019 kutohudhuria licha ya kujua tarehe ya kesi yao.
Huruma Shaidi, Hakimu Mkazi Mkuu amemtaka Mrakibu Msaidizi (ASP), Shamila Mkoma kufika mahakamani hapo tarehe 9 Aprili 2019 kutoa ushahidi dhidi ya Zitto.
Mahakamani hapo Wakili wa Zitto, Steven Mwakibolwa amedai kuwa, alipewa taarifa kwamba mteja wake (Zitto) kutoka kwa shemeji wa mteja wake Vicent Kasala kwamba Zitto anaumwa.
Na kwamba, pamoja na taarifa za ugonjwa huo wakili huyo ameeleza kuwa, hafahamu alipo Zitto.
“Kasala amenieleza kwamba mkewe Zitto kampigia kumfahamisha kwamba ni mgonjwa lakini hajui yuko wapi” amedai wakili huyo.
“Umepewa taarifa kwamba mshtakiwa anaumwa lakini huna uhakika, tusitafutane maneno hapa, siku ya kesi wadhamini na mshtakiwa waje hapa mahakamani kujieleza kwanini hawakufika mahakamani” amesema Hakimu Shaidi.
Wankyo Simon, Wakili wa Serikali ameiambia mahakama kuwa, kesi hiyo ilipangwa kuanza kusikiliza ushahidi ambapo Jamhuri iliita shahidi mmoja na kwamba, mshtakiwa hakuwepo mahakamani.
Kesi hiyo itaanza kusikilizwa ushahidi wa Jamhuri tarehe 9 Aprili mwaka huu.
Leave a comment