SIO jambo la kawaida kwa viongozi wa serikali kutwangana Makonde hadharani lakini hii imetokea katika Halmashauri ya Wilaya ya Mwanga mkoani Kilimanjaro. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa kutoka kwa maofisa wa halmashauri hiyo wilayani hapo zinaeleza kuwa, Zefrin Lubuva ambaye ni mkurugenzi wa wilaya hiyo na ofisa usalama wa wilaya hiyo Abdi Mussa walichapana kutokana na mgogoro wa kiuongozi.
Tukio hilo lilitokea kwenye ofisi ya mkurugenzi huyo baada ya kuelezwa kuwepo kwa ‘bifu’ la muda mrefu kati yao pia likimuhusisha mkuu wa wilaya hiyo Aeron Mbogho.
Kabla ya mkong’oto kati ya Mussa na Lubuva, Mbogho alimsweka ndani Lubuva kwa madai ya kushindwa kutekeleza maagizo yake.
“Hapa kuna tatizo kubwa kati ya ofisa usalama wa wilaya, mkuu wa wilaya na mkurugenzi. Uongozi wa hapa ni wa kuviziana na hakuna ushirikiano, kinachoezakutokea hapa ni matatizo makubwa kama jambo hili halitotazwamwa vema,” ameeleza ofisa mmoja wa halmashauri hiyo aliyeomba kuhifadhiwa jina lake na kuongeza;
“Hili bifu sijui limetokana na nini. Ninachojua mimi hawa watu hawafanyi kazi pamoja, aliyosema rais (Rais John Magufuli) kuhusu watumishi wa eneo moja kutoelewana ni kweli na huu ndio uthibitisho.”
Taarifa kutoka ndani ya ofisi za mkurugenzi huyo zinaeleza kuwa, mapema asubuhi ya jana tarehe 17 Januari 2019 kulikuwa na kikao ambacho mkurugenzi huyo alipaswa kuwepo.
Kutakana na kile kilichoelezwa kubanwa na majukumu yake siku hiyo, mkurugenzi huyo alilazimika kutumwa mwakilishi, jambo hilo ndio lililomkera ofisa usalama huyo na kuamua kumfuata ofisini kwake ili kumuhoji.
Baada ya majibizano ya hapa na pale na kushindwa kuelewana ndio wakaanza kurushiana ngumi. “Tulianza kusikia purukushani humo ndani na kwa busara baadhi yetu ndio walioingilia kati ili kutuliza hasira zao, ni kama watu waliokuwa wanawindana vile,” ameeleza mtoa taarifa.
Hata hivyo Mbogho (Mkuu wa Wilaya) ambaye ndiye Mwenyekiti wa Usalama wa Wilaya hiyo, alidai kutojua lolote.
Leave a comment