SOPHIA Mwakagenda, Mbunge viti Maalumu, amewapa mbinu za ushindi wajumbe wa Baraza la Wanawake la Chama cha Chadema (Bawacha), kwenye Uchaguzi Mkuu wa Mwezi Oktoba 2020. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akizungumza na wajumbe hao katika ziara ya kujifunza shughuli za bunge jana tarehe 7 Februari 2020 jijini Dodoma, Mwakagenda amewataka wajiamini pamoja na kujitokeza kwa wingi kushiriki kwenye uchaguzi huo.
Mwakagenda amewataka kuhakikisha wanaingia kwenye ushindani kugombea nafasi za ubunge, udiwani na urais. Na kuacha tabia ya kuwa wasindikizaji na wapiga debe, kutokana na hofu ya kuchuana katika uchaguzi huo.
“Ili muweze kupata ushindi kupitia chama chetu cha Chadema kwenye uchaguzi mkuu wa ngazi ya urais,ubunge na udiwani, utakaofanyika mwaka huu wa 2020 ,ni muhimu kwanza mjiamini nyinyi wenyewe. ikiwa na pamoja na kujitokeza kwa wingi kujiandikisha na kupiga kura,”amesema Mwakagenda.
Kuhusu ziara hiyo, Mwakagenda amewataka viongozi wa baraza hilo na wajumbe wake, kuitumia kama chachu ya kujiimarisha.
“Ziara kama hizi ni fursa kwenu ya kujifunza, hivyo ninawaomba muitumie kwa malengo ya kujiimarisha kimaendeleo kwenye maeneo yenu mnayotoka na kwa masilahi ya chama chetu, na sivyo vinginevyo”amesema Mwakagenda.
Kwa upande wake Kissa Swilla, kutoka Jiji la Mbeya Kata ya Ilomba akizungumza kwa niaba ya wanawake hao, ameiomba serikali kuhakikisha uchaguzi huo unakuwa huru na wa haki. Kwa kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi.
Leave a comment