SERIKALI imetoa onyo kutokana na kushamiri kwa vitendo vya rushwa ya ngono katika vyuo vya elimu ya juu. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Dk. John Jingu, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto amesema, zipo taarifa kwamba wahadhiri wengi wamekuwa wakitumia madaraka yao ‘kuwala’ wanachuo ili wawafaulishe.
Akizungumza kwenye ufunguzi wa kikao kilichowakutanisha wakuu wa vyuo vya elimu ya juu, kilicholenga mapambano dhidi ya ukatili wa kijinsia vyuo vya elimu ya juu tarehe 23 Desemba 2019, Dk. John Jingu amesema, wadhadhiri wamekuwa wakilazimisha wanafunzi kufanya nao ngono.
Amesema, imebainika kwamba si wanafunzi wote wanaopenda ama kujirahisisha kutenda vitendo hivyo, bali wahadhiri ndio wamekuwa wakitumia mwanya wa mamlaka yao kushawishi ili kukubaliwa.
Aemefafanua kwamba, hata wafanyakazi katika vyuo vya elimu ya juu, nao wamakumbwa na mkondo huo wa ukatili.
“Tunapaswa kukemea tabia hii. Tumeshuhudia vitendo vya namna hii kuwepo kwenye vyuo vyetu,” amesema Dk. Jingu.
Amewataka wakuu wa vyuo kuanzisha madawati ya jinsia katika vyuo vyao, ili kuondokana na vitendo vya kikatili na kujenga mazingira yaliyo salama katika vyuo.
Leave a comment