MIGOGORO, kutoelewana na tuhuma za ushirikina kwa wafanyakazi wa serikali zimekuwa zikisababisha kupungua kwa ufanisi katika utendaji kazi ofisini. Anaripoti Mwandishi Maalum … (endelea).
Akihutubia wananchi kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika tarehe 20 Februari 2019 katika viwanja vya Shule ya Msingi Nyakanazi, Biharamulo mkoani Kagera Kasim Majaliwa, Waziri Mkuu ameeleza kukerwa na tabia hizo kutamalaki kwa watumishi wilayanyi humo.
Waziri Majaliwa ameeleza kuwepo kwa mgogoro kati ya Saada Malunde, Mkuu wa Wilaya ya Biharamulo na Wende Ng’ahara, Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo na kwamba, hawafanyi kazi kwa ushirikiano.
Amesema, viongozi hao imefikia hatua ya kutuhumiana kutendeana vitendo vya kishirikina jambo ambalo linazidisha mgogoro baina yao.
Na kwamba, Malunde na Ng’ahara wameshindwa kufanya kazi pamoja kutokana na kutuhumiana jambo ambalo limesababisha ufanisi wa kazi kupungua.
Waziri Majaliwa amewataka kukaa pamoja na kumaliza tofauti zao na kwamba, wakishindwa kufanya hivyo atalazimia kumshauri Rais John Magufuli kufanya uamuzi wowote dhidi yao.
“Kuendeleza migogoro kunaleta taswira mbaya hasa kwa wafanyakazi walio chini ya serikali…migogoro inazorotesha maendeleo na huduma kwa wananchi,” amesema Waziri Majaliwa.
Amewataka viongozi hao kuzingatia kwamba, wameteuliwa na kupelekwa kwenye wilaya hiyo na Rais Magufuli kwa ajili ya kuwatumikia wananchi na si vinginevyo.
Leave a comment