CHARITY Ngwala (28), Ofisa Msaidizi wa Kodi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), H 4810 PC Ramadhani Uweza (28) na H 48 86 PC Simon Sugu (26) ambao ni askari polisi wa Kituo cha Polisi cha Osterbay, wamepandishwa kizimbani leo tarehe 10 Juni 2019. Anaripoti Faki Sosi … (endelea).
Maofisa hao wamepandishwa kizimbani na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kwa tuhuma za kuomba rushwa ya Sh. 2 Milioni.
Akisoma hati ya mashtaka, wakili wa serikali kutoka Takukuru, Sofia Ngula amedai mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi kuwa, tarehe 29 Oktoba 2016 Kimara Mwisho, jijini Dar es Salaam washtakiwa hao walishawishi rushwa ya Sh. 2 Milioni kutoka kwa mfanyabiashara wa Karikaoo, Ramadhani Ntunzwe.
Maofisa hao walimshawishi Ntunzwe ili waachie mizigo yake kwa madai kuwa, alifanya udanganyifu wa bidhaa alizonazo na hivyo kuathiri ukadiriaji wa kodi, kazi ambayo ni ya mwajiriwa wake.
Hata hivyo, washtakiwa wamekana shtaka hilo na wameachiwa kwa dhamana baada ya kutimiza masharti yaliyowekwa na mahakama ambapo wametakiwa kuwa na mdhamini moja mwenye kitambulisho, atakayesaini bondi ya Sh. 5 milioni.
Kwa mujibu wa upanda wa mashtaka, upelelezi katika kesi hiyo haujakamilika na wako katika hatua za mwisho kukamilisha. Kesi imeahirishwa hadi tarehe 10 Julai mwaka huu.
Leave a comment