SERIKALI imesema, bado inaangalia uwezekano kwa Watanzania waishio nje ya nchi, kupiga kura katika chaguzi mbalimbali zijazo. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Kauli hiyo imetolewa leo tarehe 23 Mei 2019, bungeni jijini Dodoma na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa wakati akijibu swali la Asha Abdul Juma, mbunge viti maalum (CCM) aliyehoji, lini serikali itakamilisha utaratibu wa kuwezesha Watanzania wanaoishi nje kupata nafasi ya kupiga kura?
Akijibu swali hilo Waziri Majaliwa amesema, serikali inaendelea kuona kama utaratibu uliopo sasa unafaa kwa Watanzania hao kupiga kura.
Hata hivyo, amesema kabla ya kuruhusu raia hao kupiga kura, serikali itafuatilia mienendo ya Watanzania waishio nje ya nchi ikiwemo shughuli zao na kama bado wana uraia wa Tanzania au wameomba uraia wa nchi husika walizoko.
“Jambo hili ni la kisera, serikali imeendelea kuona utaratibu huo kama unaweza kufaa. Sababu lazima tupate kujua nani yuko nje ya nchi, wanafanya shughuli gani na kama ni bado Watanzania au waliomba uraia wa nchi za nje.
“Na pindi sera hii itakapokamilika tutakapoona inafaa, tutakuja kujulisha Bunge na Watanzania pale inapofaa,” amesema Waziri Majaliwa.
Leave a comment