WABUNGE wameelezwa kuwa kiasi cha Sh. 20 bilioni hazikutumika ambazo ni za mfuko wa pamoja wa afya ujulikanao kama ‘Basket Fund’ kwa mwaka 2016/17, anaandika Dany Tibason.
Kufuatia hali hiyo, Wabunge wametakiwa kuhakikisha wanawabana Waganga wakuu wa Wilaya na wahasibu katika halmashauri zao ili fedha za mfuko huo zitumike kununulia dawa na vifaa tiba.
Kauli hiyo ilitolewa na Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tamisemi, Seleman Jafo alipokuwa akijibu swali la Mbunge wa Viti Maalum (CCM), Ester Mahawe.
Mahawe alitaka kujua iwapo serikali haioni umuhimu wa kupandisha bajeti ya Hospitali za Wilaya zilizoko mkoani Manyara ambazo zimekuwa zikipata ugumu katika kutoa huduma kwa wananchi.
“Vituo vya Afya na Zahanati zilizo karibu na Hospitali za Wilaya zina changamoto ya utoaji huduma bora kwa sababu ya upungufu wa dawa na watumishi wa kada ya afya hivyo kupeleka kuhudumiwa na hospitali za Wilaya ambazo bajeti ya dawa haikidhi mahitaji,” amesema Mahawe.
Akijibu maswali hayo kwa pamoja, Jafo amesema kuna tatizo la usimamizi wa rasilimali fedha ambapo katika mwaka 2016/17 mpaka mwezi wa saba kuna fedha za mfuko huo hazijatumika ambazo ni jumla ya Sh. 20 bilioni.
Alitaja mkoa wa Manyara pekee kuwa takriban Sh. 500 milioni hadi mwezi wa saba mwaka jana zilikuwa hazijatumika jambo linaloonyesha kuwa kuna mambo aliyoyaita ya hovyo kwa baadhi ya watumishi katika halmashauri mbalimbali nchini.
Leave a comment