JOHN Mongella, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, amemshauri Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Charles Tizeba kuivunja Bodi ya Pamba kanda ya ziwa kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake ipaswavyo, anaandika Moses Mseti.
Mongella amesema bodi ya pamba imekuwa kikwazo kikubwa katika harakati za kilimo cha zao la pamba nchini jambo ambalo linasababisha wakulima nchini kukata tamaa ya kulima pamba.
Kauli hiyo ameitoa leo kwenye kikao cha utekelezaji wa kilimo cha pamba katika mkoa wa Mwanza kwa msimu wa 2016/2017 na mapendekezo ya kuendeleza kilimo hicho msimu mpya wa 2017/2018 kilichowahusisha pia wadau wa tasnia ya pamba.
Mongella amesema mamlaka inayohusika na uundaji na yenye mamlaka ya kuvunja bodi ya pamba inapaswa kuichukulia hatua ikiwa ni pamoja na kuifuta bodi hiyo inayosababisha kilimo cha pamba kuendelea kusuasua na kuikosesha Serikali mapato.
Amesema bodi hiyo imekuwa ikichelewa kupeleka mbegu ya pamba na dawa ya viuatilifu kwa wakulima hatua ambayo inasababisha mavuno kidogo ya pamba katika kipindi cha hivi karibuni kwenye wilaya za mkoa huo.
“Kama mimi ningekuwa na mamlaka ya kuifuta bodi hii (bodi ya pamba) sasa hivi ningekuwa nimeifuta na wachawi wanaoiuwa pamba ni nyie na tusipokuwa makini sijui kama tutakuwa na pamba.
“Waziri (Charles Tizeba) aliizuia fedha ya mfuko wa wakfu kukatwa kwa mawakala na wanunuzi wa pamba lakini nyie bodi ya pamba mnaikata inamaana siku hiyo hamkuwepo na hamkuelewa au nyie ni viziwi,” amesema Mongella.
Mongella ameiagiza bodi ya pamba kuhakikisha mwishoni wa mwezi huu wawe tayari wamekwisha peleka mbegu ya pamba kwa wakulima na kwamba kama hawata fanya hivyo hatua nyingine zitachukuliwa kwao.
Pia Mongella aliongeza kwamba mkoa wa mwanza kumekuwepo na makampuni mengi ya ubabaishaji yanayohusika na ununuzi wa pamba huku akidai yanaendelea kuwanyonya wakulima wa zao hilo linalolimwa hususani mikoa ya kanda ya ziwa.
Gabriel Mwalo, Mkurugenzi wa Fedha na Utawala Bodi ya Pamba, amedai waziri mwenye dhamana hiyo hakuzuia bodi kukata fedha za wakfu na kwamba maelekezo yanayosemwa na Mongella hayakutolewa na waziri huyo.
Uzalishaji wa zao la Pamba Mkoa wa Mwanza umeendelea kushuka hadi kufikia takribani tani 11, 616 za pamba mbegu msimu wa kilimo wa mwaka 2014/2015 na tani 5, 037.43 msimu wa kilimo wa mwaka 2015/2016.
Leave a comment