RAIS wa Zanzibar, Hussein Mwinyi amesema, katika kipindi kifupi alichokaa madarakani, amebaini ubadhirifu wa fedha za umma katika taasisi za Serikali. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Kiongozi huyo wa Zanzibar amebainisha hayo leo Jumanne tarehe 29 Desemba 2020, katika maadhimisho ya siku ya maadili na haki za binadamu, yaliyofanyika visiwani humo.
Mwenyekiti huyo wa Baraza la Mapinduzi Zanzibar amesema, fedha nyingi za miradi ya maendeleo hazijatumika vizuri.
“Iko miradi mikubwa sana yenye fedha nyingi, fedha hazijatumika vizuri. Hivyo, mimi nadhamiria kuchukua hatua na nataka vyombo vyote vilivyoko hapa mnisaidie kuchukua hatua, tutawagusa watu wote. Hilo halina shaka,” amesema Rais Mwinyi.
Hadi leo, Rais Mwinyi ameoiongoza Zanzibar kwa siku 57, tangu alivyoingia madarakani tarehe 2 Novemba 2020, baada ya kuapishwa kuwa Rais wa Zanzibar akichukua nafasi iliyoachwa wazi na Dk. Ali Mohamed Shein ambaye alistaafu kwa mujibu wa Katiba.
Kufuatia ushindi wake wa nafasi hiyo katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 27 na 28 Oktoba 2020.
Kutokana na makosa hayo, Rais Mwinyi amesema, Serikali yake haitosita kuwachukulia hatua watu watakaobainika kuhusika nayo.
“Lakini kipindi kifupi sana nilichokua naangalia taasisi mbalimbali, makosa ni mengi, ubadhirifu ni mwingi, wizi ni mwingi. Tukisema tusichukue hatua kwa sababu tunaoneana muhali, hatutokwenda kokote,” amesema Rais Mwinyi.
Rais Mwinyi amesema “mambo haya tunayotaka kufanya, huwezi kufurahisha wote, kwa hivyo tukubali kwamba wako wengi tutakaowagusa. Nilisema nchi yetu ina tatizo kubwa la muhali, tukioneana muhali hatutajenga. Kwa hivyo naomba mnivumilie.”
Rais Mwinyi ameagiza Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali Zanzibar, kuongeza juhudi katika kusimamia matumizi ya fedha za umma katika taasisi za Serikali, ili kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha.
“Wananchi hawatafahamu pesa nyingi za Serikali zinapotea, lakini kuna ofisi ya CAG na sasa kuna watendaji wa kutosha,” amesema Rais Mwinyi.
Pia, Rais Mwinyi ameagiza Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtka visiwani humo (DPP), kuondoa changamoto zinazokwamisha ushahidi katika kesi mbalimbali.
“Haitakuwa na maana kuwepo kwa ofisi ya DDP, yenye kulalamikiwa kuwa kikwazo kwa ushahidi katika kesi mbalimbali,” amesema Rais Mwinyi.
Kuhusu maadhimisho ya siku ya maadili na haki za binadamu, Rais Mwinyi ameahidi Serikali yake kupitia taasisi zake, itaendelea kutekeleza majukumu yake kwa kufuata misingi ya utawala bora.
“Serikali itahakikisha kila mmoja anawajibika ipasavyo kutekeleza majukumu yake, ili malengo ya utawala bora yapatikane na wananchi wapate maendeleo,” amesema Rais Mwinyi
Tumesikia maneno. Sasa tunasubiri vitendo. Lini watakamatwa na kufikishwa mahakamani?