MSHAMBULIAJI wa Yanga, Saidi Ntibanzokiza huenda akaukosa mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Tanzania Prisons, kutokana na kuumia kwenye mchezo uliopita dhidi ya Ihefu FC ambao Yanga waliibuka na ushindi wa mabao 3-0. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Kocha wa klabu ya Yanga, Cedric Kaze amesema kuwa mchezaji huyo pamoja na Yacouba Sogne walipata maumivu kwenye mchezo ulipita na mpaka sasa hawajalejea mazoezini lakini wanasiku moja tu ya kesho kwa ajili ya kuwatazama kama wataweza kuwatumia kwenye mchezo ujao dhidi ya Prisons.
“Wachezaji wapo vizuri, ila wapo watatu ambao wameumia akiwemo Kabwili, Ntibanzonkiza na Yacouba waliumia kwenye mechi ya Ihefu, tutaangalia mazoezi ya kesho kuangalia kama wataweza kurudi kwenye hali yao ya kawaida ili tuweze kuwatumia” alisema Kaze.
Mchezaji huyo ambaye alijiunga na Yanga kwenye dirisha dogo la usajili, amecheza michezo miwili ya Ligi kuu na kufanikiwa kufunga bao moja na kutoa pasi nne zilizo zaa mabao manne.
Kiwango alichokionesha Ntibanzokiza kwenye michezo miwili ya Ligi, huenda kukawapa hofu mashabiki na wapenzi wa klabu hiyo kwa kukosa mchango wake kwenye mchezo huo muhimu.
Yanga kwa sasa imeweka kambi jijini Mbeya kwa ajili ya kujiandaa na mchezo huo dhidi ya Tanzania Prisons utakaochezwa kwenye Uwanja wa Nelson Mandela uliopo Sumbawanga siku ya Alhamisi tarehe 31 Desemba, 2020 majira ya saa 10 jioni.
Mpaka sasa Yanga imecheza michezo 17 ya mzunguko wa kwanza bila kupoteza mechi yoyote, huku ikijikita kileleni mwa msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 43, huku nafasi ya pili ikishikwa na Simba yenye pointi 32, ikiwa na michezo mitatu mkononi.
Leave a comment