RAIS John Magufuli amesema, ili maendeleo yapatikane wakati mwingine lazima nguvu itumike. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo tarehe 11 Aprili 2019 wakati akihutubia wananchi katika ziara yake ya kikazi mkoani Njombe.
Alitoa kauli hiyo wakati akizungumzia changamoto ya baadhi ya wahandisi wa wizara ya maji kutotekeleza majukumu yao ipasavyo, na kusababisha kusua sua kwa ukamilikaji wa miradi ya maji kitendo kinachosababisha wananchi kutaabika na adha ya ukosefu wa maji safi na salama.
“Saa nyingine kuyapata maendeleo lazima nguvu iwepo, ukipeleka pole pole, ukibembeleza hata kama mtoto unataka kumpa yai anaweza asile, muweke kibao uone kama hatalimaliza kulila, atalibugia haraka haraka,
mwanangu kunywa uji, kwanza mtoto atakuwa ana kiburi anaweza kikombe akakitupa na kugalagala hebu muwashe kibao kidogo, uji ule ataunywa mpaka utadondokea kwenye shingo. Sasa ni lazima sisi viongozi wa wizara tusimamaie vizuri watendaji wetu ili miradi hii inayo gharamiwa na fedha nyingi za wananchi ilete maendeleo kwa wananchi,” amesema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli ameagiza wahandisi wote wa maji wa Halmashauri wahamishiwe katika Wizara ya Maji na Umwagiliaji kuongeza ufanisi kwenye utekelezaji wa miradi ya maji.
“Mainjinia wote wa halmshauri za wilaya wote wa Tanzania nzima wahamie wizara ya maji, ili miradi yote iweze kutengenezwa badala ya kukaa kule na kuzungumza miradi iliyoko katika makaratasi, nimeona nizungumze sababu sasa hivi tumepata fedha nyingi katika miradi ya maji ,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment