SALIM Abdullah Turky (57), mbunge anayemaliza muda wake katika jimbo la Mpendae, Unguja, kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM), amefariki dunia. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Turky ambaye afahamika kwa jina maarufu la Mr White, alikutwa na mauti usiku wa kuamkia leo, tarehe 15 Septemba, mjini Unguja.
Alikuwa mbunge wa Mpendaye aliyechaguliwa katika uchaguzi mkuu wa 25 Oktoba 2015 na kutumikia nafasi hiyo, hadi mauti yanamkuta. Katika uchaguzi mkuu wa Oktoba 28 mwaka huu, Turky alipitishwa na chama chake, kugombea tena nafasi hiyo.
Katibu wa Halmashauri Kuu ya taifa (NEC) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Humphrey Polepole, amethibitisha kufariki dunia kwa mwanasiasa huyo mashuhuri Visiwani Zanzibar.
“…tumepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za kifo cha Ndg. Salim Abdullah Turky (Mr White), mgombea ubunge wa CCM, jimbo la Mpendae, Zanzibar,” ameeleza Polepole kupitia ukurasa wake wa twitter.
Akaongeza, “tunatoa salamu za pole kwa familia, wanaCCM, wadau wa sekta binafsi nchini na wote walioguswa na msiba huu….”
Salim Hassan Turky, aliyezaliwa 11 Februari 1963, mjini Unguja, anatarajiwa kuzikwa jioni ya leo, kijijini kwake, Fumba, takribani umbali wa kilomita 65 kutoka jimboni kwake, Mpendae, wilaya ya Mjini Magharibi.
Wakati wa uhai wake, hasa alipokuwa bungeni, Turky alikuwa miongoni mwa wabunge wachache, waliojitambulisha kuwa wawakilishi wa wananchi, kwa kutoweka mbele itikadi za kisiasa.
Atakumbukwa na wengi kwa mchango wake mkubwa aliyoutoa wakati wa shambulio dhidi ya aliyekuwa mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu.
Ni Turky aliyedhamini malipo ya ndege iliyomchukua Lissu kutoka uwanja wa ndege wa kimataifa wa Dodoma hadi Nairobi, nchini Kenya.
Mwenyezi Mungu amlaze mahali pema peponi – Amin.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online, MwanaHALISI TV na mitandao yetu ya kijamii kwa habari na taarifa zaidi
Leave a comment