KIUNGO mshambuliaji wa Klabu ya Leicester City inayoshiriki Ligi Kuu England na Timu ya Taifa ya Algeria, Lihard Mahrez amefanikiwa kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka barani Afrika zilizotolewa katika mji wa Abuja, Nigeria kwa kuwashinda Emerick Aubameyang wa Gabon na Sadio Mane wa Senegal.
Mahrez ambaye alikuwa na msimu mzuri kwenye klabu yake ya Leicester City, baada ya kuisaidia kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu ya England ametwaa tuzo hiyo kwa mara ya kwanza, toka alipoanza kucheza soka katika maisha yake.
Baada ya kuchukua tuzo mchezaji huyo amesema haikuwa rahisi kiasi hicho kwa yeye kuchukua tuzo kubwa kama hiyo.
“Haikuwa rahisi kushinda tuzo kubwa kama hii, tena nina furaha kushinda mbele ya wachezaji wenye majina makubwa,” amesema Mahrez.
Hii itakuwa tuzo yake ya tatu toka kumalizika kwa msimu uliopita baada ya kushinda tuzo ya mchezaji bora wa kulipwa wa mwaka nchini England (PFA) na ile ya mchezaji bora wa mwaka kwa Afrika inayotolewa na chombo cha habari cha BBC.
Tuzo nyingine zilizotoka usiku huo zilienda kwa Alex Iwob (20) anayechezea klabu ya Arsenal na timu ya taifa ya Nigeria, alishinda tuzo ya mchezaji bora mwenye umri mdogo na tuzo nyingine ikaenda kwa golikipa timu ya Taifa ya Uganda na Mamelods Sundowns FC ya Afrika Kusini, Denis Onyango ambaye alishinda tuzo ya mchezaji bora wa mwaka kwa wanaocheza ndani ya bara la Afrika.
Leave a comment