Friday , 26 April 2024
Home Gazeti Habari za Siasa Magufuli: Uchaguzi umekwisha, tulijenge Taifa
Habari za Siasa

Magufuli: Uchaguzi umekwisha, tulijenge Taifa

Spread the love

JOHN Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amewaeleza wananchi wa Taifa hilo uchaguzi mkuu umemalizika na jukumu lililopo mbele ni kuwatumikia wananchi. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).

Rais Magufuli amesema hayo leo Alhamisi tarehe 5 Novemba 2020 baada ya kuapishwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma kuwa Rais wa Taifa hilo, sherehe iliyofanyika Uwanja wa Jamhuri Dodoma.

Pia, Samia Suluhu Hassan, ameapishwa kuwa Makamu wa Rais wa Tanzania ambao kwa pamoja watawaongoza Watanzania kwa kipindi kingine cha miaka mitano 2020-2025.

Dk. Magufuli ameapishwa baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kumtangaza mshindi wa urais katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano ya tarehe 28 Oktoba 2020 kwa kupata kura milioni 12 kati ya milioni 15 zilizopigwa sawa na asilimia 84.

Mshindani wake wa karibu, Tundu Lissu wa Chadema alipata kura milioni 1.9 sawa na asilimia 13.

Rais Magufuli ametumia dakika 16 pekee kuwahutubia viongozi mbalimbali wa ndani na nje ya Tanzania pamoja na wananchi waliohudhulia sherehe hizo za kwanza za uapisho wa Rais kufanyika jijini Dodoma.

Amewashukuru watu mbalimbali waliojitokeza kwenye sherehe hizo, “nawashukuru sana na mimi kuwa Rais wa kwanza kuapishwa katika hili Jiji la Dodoma.”

Huku akishangiliwa, Rais Magufuli amesema “nawashukuru Watanzania wenzangu kwa kuniamini na kunichagua ili niwaongoze kwa miaka mitano na kukipa ushindi mkubwa chama changu cha mapinduzi na ushindi huu si wa wana CCM pekee bali ni wa Watanzania wote”

Pia, ameipongeza, Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kwa “kusimamia uchaguzi huu” pamoja na kuvishukuru vyombo vya ulinzi na usalama kwa kudumisha amani kabla na baada ya uchaguzi.

Rais Magufuli amesema, baadhi ya nchi, uchaguzi umekuwa chanzo cha mgogoro na uhasama, “sisi Watanzania tumevuka salama na hii ni ishara kwamba mwenyezi Mungu ametuvusha salama kama alivyotuvusha kwenye janga corona.”

“Nawashukuru viongozi wa mataifa mbalimbali waliokuja kuungana nasi, wapo marais, mawaziri wakuu, mawaziri na mabalozi wote na wawakilishi wa taasisi za mataifa kama EAC na SADC,” amesema Rais Magufuli.

Kiongozi huyo amesema “uchaguzi sasa umekwisha, uchaguzi sasa umekwisha, uchaguzi sasa umekwisha na jukumu kubwa na muhimu lililopo mbele ni kulijenga na kuleta maendeleo taifa letu na niwahakikishe Watanzania, kiapo nilichoapa na makamu wang (Samia Suluhu Hassan), tutakienzi.”

Amesema, watawatumikia wananchi “bila kujali tofauti zetu, dini, kabila, kisiasa, nitashirikiana nanyi nyote ili yale niliyoyaahidi nayakumbuka yapo kwenye Ilani yetu-CCM na kuendelea kudumisha amani na usalama, uhuru wa nchi yetu bila kusahau Muungano na kuenzi mapindu matukufu ya Zanzibar.”

Rais Magufuli amesema, katika uongozi wa miaka mitano, watasimamia kumaliza miradi “tuliyoianzisha, kusimamia rasilimali mbalimbali za taifa, kushughulikia tatizo la ajira hususan vijana na kero zinazowakabili wananchi, tutazidisha mapambano ya rushwa na ufisadi.”

Ametumia fursa hiyo kuvishukuru vyombo vya habari kwa kazi kubwa waliyoifanya mliyoifanya kuanzia mwanzo hadi mwisho wa kampeni, wasanii waliojitokeza kuwaombea kura pia,  “nawapongeza pia wabunge na madiwani waliochaguliwa na bahati nzuri wengi mwaka huu wanatoka Chama Cha Mapinduzi.”

Rais Magufuli aliyeanza hotuba hiyo saa 5:55 asubuhi na kuhitimisha saa 6:11 mchana amesema, “nilianza kampeni na kuzihitimisha hapa Dodoma, asanteni sana wana Dodoma na niwahakikishie wana Dodoma yote tuliyoyaahidi tutayashughulikia ikiwemo barabara ya mzunguko kwani foleni imeanza kuonekana.”

Leave a comment

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *

Related Articles

Habari za Siasa

Prof. Muhongo akomalia matumizi nishati jadidifu kuondoa uhaba wa umeme

Spread the love  MBUNGE wa Musoma Vijijini (CCM), Profesa Sospeter Muhongo, ameendelea...

Habari za Siasa

Kilosa yawa mfano wa kuigwa miradi ya Mwenge nchini

Spread the love  KIONGOZI wa Mbio za Mwenge Kitaifa Godfrey Mzava amezitaka...

Habari za SiasaTangulizi

Biteko ataja vipaumbele 7 bajeti nishati 2024/25

Spread the love  NAIBU Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto...

Habari MchanganyikoHabari za Siasa

Mwekezaji amwaga bil. 39 kujenga viwanda 3 vya uchenjuaji

Spread the loveKampuni ya Mineral Access System Limited (MAST) inayoiwakilishwa kampuni ya...

error: Content is protected !!