TUNDU Lissu, Mbunge wa Singida Mashariki (Chadema), muda huu atafanyiwa upasuaji mwingine katika mguu wake wa kulia, ikiwa ni mara ya 20 tangu alipoanza kutibiwa baada ya kushambuliwa kwa risasi. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Lissu amesambaza ujumbe katika mitandao ya kijamii ulioeleza: “Napenda kuwajulisha kwamba ndani ya nusu saa ijayo ninaingia kwenye operesheni nyingine tena.”
Amesema madaktari wamebaini bakteria katika mguu wake wa kulia ambao uliumizwa sana, hivyo wameamua kumfanyia upasuaji ili kuwaondoa.
Operesheni hiyo inayofanyika nchini Ubelgiji ni ya 20 baada ya ile ya 19 ilifanyika mwezi Machi mwaka huu ikiwa ni mwendelezo wa matibabu aliyokuwa akifanyiwa katika Hospitali ya Nairobi nchini Kenya alikopelekwa akitokea Dodoma baada ya kushambuliwa kwa risasi zaidi ya 30 akiwa nje ya makazi yake mjini Dodoma Septemba 7, mwaka jana.
Lissu amesema baada ya operesheni huo atafanyiwa upasuaji mwingine baadaye wa kuunga mfupa. “Niseme tu naendelea vizuri sana. Ninawashukuru Watanzania kwa kunitibu, kwani wenye jukumu la kufanya hivyo wamekataa lakini Watanzania hawajanitupa.”
Leave a comment