ALIYEKUWA mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), nchini Tanzania, Godbless Lema amekimbilia nchini Kenya, ili kuomba hifadhi ya kisiasa, katika ubalozi wa Marekani, jijini Nairobi, Kenya. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Taarifa kutoka nchini Kenya zinasema, Lema alivuka mpaka wa Tanzania na kuingia nchini humo, Jana Jumamosi.
Hata hivyo, alikamatwa na Polisi katika Kaunti ya Kajiando baada ya yeye na familia yake kuvuka mpaka wa Namanga, kinyume cha taratibu.
Kwa mujibu wa tovuti ya The Standard Media ya Kenya, Lema alikuwa na mkewe, Neema Godbless na watoto wao watatu.
Kupatikana kwa taarifa za Lema amekimbilia nchini Kenya kuomba hifadhi ya kisiasa, kunakuja takribani siku sita, tangu mwanasiasa mwingine wa upinzani nchini Tanzania kuomba hifadhi ya kisiasa, akihofia usalama wa maisha yake.
Tundu Lissu ambaye alikuwa mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yuko katika makazi ya balozi wa Ujerumani jijini Dar es Salaam, akiomba hifadhi kwa kile alichoita, “kuhofia” usalama wake.
Akizungumza na gazeti la hilo, Lema alisema maafisa wa uhamiaji walikataa kugonga muhuri nyaraka zilizowasilishwa na mke wake, kwa madai hadi wamuone yeye.
Amesema, mke wake alipomuita alikwenda, lakini akawaambia hana hati yake ya kusafıria kwa sababu alikuwa hasafıri na kwamba mke na wanae walikuwa wanakwenda kutafuta shule ya kimataifa nchini Kenya.
Maafisa waliruhusu mke na watoto kuvuka mpaka na Lema aliomba kwenda kutafuta fedha za Kenya ili ampe mke wake ambaye alisema angeendelea na safari yeye na watoto.
Lakini mara tu alipovuka mpaka, Lema na familia yake waliingia ndani ya gari la mwanasheria wake, George Luchiri ambaye alikuwa akifuatilia mchakato mzima wa Lema kuvuka mpaka kuingia Kenya.
Maafisa hao wa uhamiaji walitoa taarifa polisi kwamba kuna mtu ameingia nchini humo bila kuwa na nyaraka husika.
“Polisi walitufuatilia na wakatukamata tukiwa Ilbisil na kutupeleka kwenye kituo cha polisi. Sikutaka wamuweke pale Lema kutokana na ukaribu wake na mpaka wa Tanzania,” ameeleza mwanasheria huyo akinukuliwa na gazeti la The Standard.
Mwanasheria huyo amesema, alifahamu kwamba Lema anakwenda Kenya na kwamba alitaka ampeleke Tume ya Haki
za Binadamu ya Umoja wa Mataifa mara tu atakapavuka mpaka.
Luchiri amesema, kwa mujibu wa tume hiyo, mtu anayetafuta hifadhi hahitaji kuwa na nyaraka za kumuwezesha kuingia nchi nyingine.
Akieleza sababu za kutokutoa hati yake ya kusafıria, Lema amesema, alijua kwa kufanya hivyo, maafisa hao wangemshikilia na kumzuia kuvuka.
“Nimeacha kila kitu nyumbani. Hivyo havina umuhimu kwa sasa. Muhimu ni usalama wangu na usalama wa familia yangu. Nipo na wanangu Allbless, Brilliance na Terrence. Sijui kesho itakuja na nini. Kwa sasa natafuta hifadhi,” Lema ameiambia The Standard.
Mwanasheria huyo amesema atawasilisha taarifa za Lema katika Ubalozi wa Marekani kwani amekuwa akifanya mawasiliano na maafisa wa ubalozi huo.
Leave a comment