CHAMA Cha Wananchi (CUF) nchini Tanzania, kimemvua madaraka Naibu Katibu Mkuu wake Zanzibar, Ali Makame Issa kwa kosa la kwenda kinyume na msimamo wa chama hicho wa kutokubali matokeo ya Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Jumapili tarehe 8 Novemba 2020 na Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mahusiano na Umma CUF, Mhandisi Mohamed Ngulangwa imeelezea uamuzi huo.
Mhandisi Ngulangwa amesema, Issa alikwenda kinyume na msimamo wa chama hicho kwa kushiriki mchakato wa uchaguzi wa Spika na Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar.
“Jana jioni, kulikuwa na mchakato wa Kuwachagua Spika na Naibu Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, katika kukamilisha mchakato wa uchaguzi ambao sisi CUF tumeupinga na kuyakataa matokeo yake.”
“Kinyume na matarajio ya viongezi na wanachama wa CUF, Issa alikuwa ni miongoni mwa waliojitokeza kugombea nafasi ya Spika wa Baraza la Wawakilishi, nje ya ridhaa ya chama,” amesema Mhandisi Ngulangwa.
“Issa ni miongoni mwa wajumbe wa Kamati Tendaji na pia ni Mjumbe wa Kamati ya Uongozi aliyeshiriki vikao vilivyopitisha Maamuzi ya Msimamo wa Chama kuhusu Uchaguzi Mkuu ulioharibiwa.”

Taarifa hiyo ya Mhandisi Ngulangwa imesema “Isitoshe, ni miongoni mwa Viongozi Waandamizi waliokuwa pamoja na Msemaji Mkuu wa Chama ( Mwenyekiti) wakati anafikisha kwenu tamko la Chama la kutoutambua Uchaguzi Mkuu.”
Amesema, CUF kimeonya viongozi wake kutokwenda kinyume na msimamo wake kuhusu uchaguzi huo.
“CUF kisingependa kuona yeyote katika viongozi wake akiiga viongozi wa vyama vingine vinavyowasaliti wananchi kwa kuunga mkono au kushirikiana na Serikali zitokanazo na ubakaji wa demokrasia ili kulinda maslahi binafsi ya vyama hivyo au viongozi wao. Dhambi hii ya kusaliti maisha na damu ya wananchi, haiwezi kuvumiliwa na CUF,” amesema Mhandisi Ngulangwa.
Aidha, chama hicho kimewaomba radhi Watanzania kufuatia ukiukwaji huo.
“Chama kinawaomba radhi Watanzania kutokana na ukakasi uliosababishwa na Ali Makame Issa kwa kujitokeza kwake hadharani kugombea nafasi ya Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar bila ya ruhusa ya chama,” inaeleza taarifa ya Ngulangwa.
Leave a comment