RAIS Mstaafu, Dk. Jakaya Kikwete, amestaajabu uzushi unaosambazwa mitandaoni kuhusu kifo cha Dk. Reginald Mengi. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Dk. Kikwete ambaye aliongoza nchi hii kuanzia 2005 hadi 2015, ameeleza kushtuwa na utunzi wa uongo kuhusu sababu za kifo cha mfanyabiashara huyo (Dk Mengi).
Amewataka Watanzania kutojenga tabia ya uzushi na kwamba, wanaofanya hivyo, waache na wawe na subira.
Dk. Mengi ambaye ni mwenyekiti wa kampuni zilizo chini ya IPP Group, alifariki usiku wa kuamkia tarehe 2 Mei 2019 akiwa Dubai, Falme za Kiarabu.
Akizungumza nyumbani kwa Marehemu Dk. Mengi, Kinondoni jijini Dar es Salaam leo tarehe 4 Mei 2019, Rais Kikwete amewataka Watanzania kuacha kuzusha taarifa za uongo juu ya chanzo cha kifo cha mfanyabiashara huyo.
Rais Kikwete amesema kuwa, si jambo jema katika msiba kuingiza maneno yasiyokuwepo kuhusu kifo cha Dk. Mengi na kwamba, kufanya hivyo kunaweza kuichanganya jamii.
Amewataka Watanzania kuwa watulivu katika kusubiri usahihi na ukweli wa sababu za kifo cha Dk. Mengi.
“Sisi wengine tuendelee kuwa watulivu, tuache uongo na kuingiza yasiyokuwepo tukaichanganya jamii, haya ya kutunga tuachane nayo, tusubiri ukweli. Alifariki akiwa Dubai na kaka yake alikuwepo,” amesema Dk. Kikwete na kuongeza;
“Haya tunayosema, tuacheni kusudi wakirudi watueleze kilichotokea, tutajua sababu. Na maneno yangu msije mkayachanganya tena.”
Mwili wa Dk. Mengi unatarajiwa kuwasili nchini Jumatatu ya wiki ijayo, kisha kuagwa Jumanne tarehe 7 Mei 2019 na baadaye kuzikwa nyumbani kwao mkoani Kilimanjaro Alhamisi tarehe 9 Mei mwaka huu.
Tazama video kamili hapo chini
Leave a comment