KANISA Katoliki Tanzania limetoa waraka uliobeba ujumbe wa Kwaresima, huku likiangazia changamoto zinazokabili familia na visababishi vya changamoto hizo. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Waraka huo uliotolewa jana na Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) umeeleza kuwepo kwa dhana potofu na nadharia zisizo sahihi zinazolenga kuhalalisha vitendo vinavyosababisha kutenganishwa kwa ndoa na familia.
Waraka huo umeainisha kuwa, zipo mila na tamaduni ambazo zinachochea uwepo wa changamoto katika familia, ikiwemo tamaduni zinazoruhusu talaka, ndoa za utotoni, uchumba sugu, ndoa za jinsia moja na ndoa baada ya ndoa halali ya kwanza.
“Sisi kama wadhambi tulio safarini kuelekea huo utakatifu, kwa mwaka huu wa 2019 baada ya kuadhimisha miaka 150 ya Kanisa Katoliki Tanzania mwaka jana, tumeona ujumbe wa mwaka huu uzingatie dhamira inayohusu familia zetu,” inaeleza sehemu ya waraka wa TEC.
Familia zenye mchanganyiko wa imani, zinazoishi katika mazingira magumu ya uchumi, familia zisizoishi imani, familia zisizo na maadili, familia zilizopoteza uwezo wa kulea na familia zisizo na kipato, ni changamoto nyingine zilizotajwa katika waraka huo.
“Ili katika kujitafakari na kuamsha upya maisha yetu ya imani Katoliki na maadili yake, tutambue zaidi na tukiri kwa dhati jinsi hali yetu ilivyo mbele ya Mungu ambaye ndiye chanzo cha utakatifu,” TEC inaeleza katika ujumbe wake huo
Waraka huo umebainisha kuwa, kuna harakati zinazopigia upatu uhuru usio wa kweli kwa mwanadamu na kupotosha ukweli kwa kutenganisha ukweli wa maisha na ukweli wa asili katika viumbe na maumbile yao.
TEC inaeleza kuwa kila mwaka hutoa ujumbe mahsusi kwa jamii katika kipindi cha Kwaresima likilenga kuionya jamii ili kuenenda katika njia sahihi.
“Dhamira hii ya familia kama kanisa la nyumbani na shule ya imani na maadili, kwa mwaka huu basi, tutafakari kwa namna gani hili lifanyike kwa kuzingatia kuwa familia ya kikristu ni shule ya imani Katoliki na maadili yake,” ianeleza sehemu ya waraka wa TEC.
Leave a comment