KATIBU Mkuu wa Chadema, Dk. Vincent Mashinji ‘amesukumwa ndani’ na wenzake saba mkoani Kilimanjaro. Anaripoti Mwandishi Wetu … (endelea).
Jeshi la Polisi mkoani humo lilitumwa kukamata viongozi hao jana kwa madai ya kufanya mkutano wa ndani bila kuruhusiwa.
Wakati Dk. Mashinji akikamatwa na jeshi hilo, Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Freeman Mbowe ameendelea kuwekwa mahabusu baada ya kukataliwa dhamana.
Mbowe anatarajiwa kufikishwa mahakamani tena jijini Dar es Salaam baada ya mwaka mpya 2019 kuingia jamba ambalo pia laweza kumkuta Dk. Mashinji.
Dk. Mashinji na viongozi wengine wa chama hicho wamekamatwa kwa amri ya Mkuu wa Wilaya ya Hai, Lengai ole Sabaya kwa madai ya kukiuka taratibu.
Kiongozi hao wa Chadema wanatuhumiwa kufanya kikao kinyume na utaratibu.
Awali taarifa zinaeleza kuwa, Mkuu huyo wa wilaya alizuia kufanyika kwa kikao cha ndani cha viongozi hao wa Chadema kwa kuwaandikia barua katika eneo la Bomang’ombe.
Hata hivyo Chadema walikutana na kuanza kikao chao cha ndani nipo Jeshi la Polisi mkoani likaenda kuwakamata.
Sabaya anathibitisha kuwa, kukamatwa kwa viongozi hao ni maagizo kutoka kwake baada ya kuendelea na kikao alichokizuia.
Sabaya amedai kwamba viongozi wa Chadema hawakufuata taratibu na kuwa, uongozi wa wilaya ulikuwa hauna taarifa.
“Ni kweli nimeagiza viongozi hao wakamatwe,” amesema Sabaya na kuongeza:
Wilaya ya Hai si sehemu ya kuja kuzurura na kufanya wapendayo.”
Leave a comment