JAJI Joseph Sinde Warioba, Waziri Mkuu Mstaafu wa Tanzania amesema, kuna dalili za uwepo wa matukio yanayodhoofisha umoja, uzalendo na mshikamano wa Taifa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Jaji Warioba amesema hayo leo tarehe 24 Septemba 2019, katika hafla ya uzinduzi wa Tamasha la 14 la Jinsia linalofanyika katika ofisi za Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP), Mabibo jijini Dar es Salaam.
“…kuna dalili za hapa na pale, ambako unaona kuna majaribu ya kudhoofisha umoja wetu, mshikamano wetu,” amesema Jaji Warioba.
Jaji Warioba amesema, nguvu ya Tanzania ni umoja, mshikamano na uzalendo na kwamba wanawake wana nafasi kubwa ya kuhakikisha nguzo hizo zinakuwa imara.
Akitolea mfano mchakato wa upatikanaji wa Katiba Mpya uliofanyika mwaka 2013, Jaji Warioba amesema wanawake walitoa mapendekezo yao bila ya kuwa na mgawanyiko wa kiitikadi ama siasa.
“Watanzania nguvu yetu iko kwenye udugu wetu, ndio nguvu tuliyonayo, na tuna amani, umoja ushirikiano na uzalendo. Ni muhimu tulinde uhuru, mshikamano wetu na uzalendo wetu. Lakini wanawake wa nchi hii, ndio ambao wana dhamana ya kulinda umoja wetu na mshikamano wetu,” amesema Jaji Warioba na kuongeza.
“Nilikwenda Bagamoyo nilikuta kuna semina ya wabunge wanawake, wanazungumza lugha moja hawakugawanyika kwamba hawa CCM, CHADEMA, CUF wanazungumza mambo ya kitaifa. Tulipokuwa na jukwaa la katiba, kikundi pekee ambacho kilitoa mapendekezo bila mgawanyiko ni wawanake.
Tamasha la 14 la Jinsia linafanyika kwa siku nne kuanzia leo hadi tarehe 27 Septemba 2019 jijini Dar es Salaam.
Tamasha hilo linawakutanisha wanaharakati wa haki za jinsia, wanasiasa na wadau mbalimbali hasa asasi za kiraia.
Leave a comment