BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imeeleza, kwamba virusi vya corona vinavyosababisha homa ya mapafu (COVID-19), havikai kwenye pesa ya Tanzania. Anaripoti Faki Sosi, Dar es Salaam … (endelea).
Imeelezwa, fedha hizo zimetengenezwa kwa mazingira ambayo vimelea hivyo haviwezi kubaki ama kuganda hata pale mtu mwenye maambuziki hayo atashika fedha hizo.
Taarifa ya benki hiyo iliyotolewa leo tarehe 19 Machi 2020, imewataka Watanzania kutokuwa na hofu kwamba fedha hizo zinaweza kuwa chanzo cha kusambaa kwa virusi hivyo.
BoT imewataka wananchi kupuuza taarifa, kwamba virusi hivyo vya COVID-19 vinaweza kuenea kupitia fedha, huku taarifa hiyo ikisisitiza wananchi kuendelea kuchukua hatua za kujikinga kwa namna inavyoelezwa na mamlaka husika (serikali).
Pia, taarifa hiyo imesisitiza wananchi kufanya kwa wingi miamala kwa kutumia njia mbadala za malipo ikiwemo simu za mkononi, intaneti bila kulazimika kwenda benki ama ATM ili kupunguza kuenea kwa COVID-19.
“Tunawashauri wananchi kuzingatia miongozo mbalimbali inayotolewa na mamlaka zenye dhamana ya afya ya jamii, ikiwa ni pamoja na kunawa mikono mara kwa mara, kutumia maji yanayotiririka na sabuni au kutumia vitakasa mikono (Sanitizers), kufanya hivyo kutasaidia kuua vimelea kwenye mikono,” imeeleza taarifa hiyo.
Leave a comment