SERIKALI imesema kuwa, enzi za kutegemea wajomba zimekwisha na sasa, Watanzania washikamane na kufanya kazi kwa bidii. Anaripoti Dandon Kaijage, Dodoma … (endelea).
Akisoma Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2019/20 jijini Dodoma leo tarehe 13 Juni 2019, Dk. Philip Mpango, Waziri wa Fedha na Mipango amesema, Watanzania wanapaswa kushikamana katika kujenga Tanzania mpya.
“Kwa Watanzania wenzangu, napenda tuendelee kusisitizana katika kuijenga Tanzania mpya. Tuwe wazalendo na tena tukae macho daima kulinda na kutetea taifa letu. Tuongeze bidi kufanya kazi, enzi za kutegemea wajomba hazipo tena,” amesema Dk. Mpango.
Akizungumzia ushirikiano na wadau wa maendeleo kutoka nje Dk. Mpango amesema, Tanzania inashukuru ushirikiano wao katika maendeleo na kwamba, wanakaribisha wawekezaji nchini.
Hata hivyo Dk. Mpango ameeleza kuwa, wawekezaji wanafunguliwa milango lakini uwekezaji huo kutokuwa na mashatri magumu.
“Serikali ya awamu ya tano inatambua na mchango ya wadau wetu wa maendeleo kwa maendeleo ya taifa letu. Tunakaribisha uwekezaji nchini ilimradi usiwe na masharti ambayo ahayendani nasi pia mila na desturi zetu. Masharti hayo yasiwe yanahatarisha uhuru wa Tanzania, amesema Dk. Mpango na kuongeza:
“Hata pale serikali na mihimili mingine inapofanya maamuzi ambayo hawakubaliani nayo, ni vema na haki washirika wetu wa maendeleo watupe muda wa kuyatafakari, na kujadiliana nao tena kwa staha badala ya kuishinikiza serikali ibadili uamuzi wake ndipo watoe fedha jambo ambalo halikubaliki hata kidogo.”
Leave a comment