ASKOFU wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dayosisi ya Karagwe mkoani Kagera amesema, “mimi niko salama, naendelea na majukumu yangu kama kawaida. Mimi si mtumishi wa umma, nitawashtaki kwa Mungu.” Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Kiongozi huyo wa kiroho, amesema maneno hayo leo Jumamosi tarehe 12 Desemba 2020 alipozungumza na MwanaHALISI Online lililotaka kujua maendeleo yake hasa baada ya uwepo wa taarifa za kutishiwa usalama wake.
Amesema, kama wiki moja iliyopita alipokea taarifa za kutishiwa, akaendelea kukaa kimya.
“Vilianza kama vituko, watu kunitumia ujumbe wa kunitishia kuwa mimi ni mpinzani, napinga serikali, ngoja nitaona, kama unafikiri mimi ni mjanja utaona, kichwa changu kitakapotenganishwa.”
“Baadaye nikapigiwa simu na watu wema, waliokatika nafasi nyeti na kuniambia niwe mwangalifu kuwa hawa watu wamepiga kambi Karagwe maaluum kwa kukushughulikiwa wewe kama walivyomfanya askafu mwenzako,” amesema Askofu Bagonza.
Amesema “siamini kwamba serikali inaweza kutuma watu wajinga namna hiyo, mimi niko salama. Niko salama na hatua zote za kuimalisha ulinzi wangu ziko vizuri.”
Askofu Bagonza amesema “naendelea kutoa huduma na hakuna jambo lolote baya nililofanya. Najifahamu tangu nikiwa mdogo, kitu pekee ninachokithamini ni uhuru wa maoni. Situkani mtu na wala sifanyi kosa.”
Akijibu kuwa amekwisha kutoa taarifa polisi, Askofu Bagonza amesema “ukiona hao watu wema walionipigia kama ni polisi sasa nakwenda kuripoti nini polisi? Ukionewa na polisi utampeleka polisi? Ikiwa watu wema walionipigia wanaweza kuwa polisi baadhi yao, sasa nakwenda kufanya nini? Mimi si mtumishi wa umma, nitawashtaki kwa Mungu.”
Leave a comment