KAMATI Kuu ya Chama cha ACT-Wazalendo, imeketi leo tarehe 2 Agosti 2020 ikiwa ni maandalizi ya kuelekea Mkutano Mkuu. Anaripoti Hamis Mguta, Dar es Salaam…(endelea).
Wakati wa ufunguzi wa kikao hicho, Janeth Rithe, Naibu Katibu Muenezi wa chama hicho ameseme, miongoni mwa ajenda kuu katika kikao hicho ni kuhusu Mkutano Mkuu unaotarajiwa kufanyika tarehe 5 Agosti 2020.
Amesema, Mkutano Mkuu ndio utakaotumika kupata majina ya wagombea urais kwa upande wa Tanzania Bara na Visiwani Zanzibar na kwamba, wagombea hao watapitishwa kutokana na sifa zao kwa chama na kwenye macho ya wapiga kura.
“Leo tunaanza na Kamati Kuu, kesho kutakuwa na Halmashauri Kuu na Jumatano tutakuwa na Mkutano Mkuu ambapo tutazindua hiyo Ilani na kutangaza wagombea wetu wa urais,” amesema.
Akizungumzia ushirikiano na vyama vingine, Janeth amesema, suala hilo bado linajadiliwa kwenye vikao vikubwa vya viongozi wakuu na kwamba, litakapokuwa tayari, litawekwa hadharani.
“Lengo letu ni sisi kama wapinzani ni kuhakikisha tuiondoa CCM madarakani, haijalishi nani ana nguvu zaidi lakini nini ambacho mtakubaliana ndio muhimu.
“Ushirikiano ni ni kiu ya wananchi na ili kutimiza kiu hiyo, sisi viongozi wa vyama vya siasa tunapaswa kufanya mazungumzo ambayo hayataleta neema kwa nchi,” amesema.
Leave a comment