SERIKALI imetangaza vifo viwili vya wagonjwa wa Homa Kali ya Mapafu, inayosababishwa na Virusi vya Corona (COVID-19). Anaripoti Hamis Mguta…(endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya, vifo hivyo vimetokea leo tarehe 10 Aprili 2020 jijini Dar es Salaam, na kufanya idadi ya vifo vitatu vilivyotokana na ugonjwa huo.
“Tunasikitika kutoa taarifa ya vifo viwili vilivyotokea leo miongoni mwa wagonjwa waliothibitishwa kuwa na maambukizi ya Corona nchini, ambavyo ni vya watanzania, mwanaume mwenye umri wa miaka 51 na mwanaume mwenye umri wa miaka 57, wote wakazi wa Dar es Salaam,” inaeleza taarifa ya Waziri Ummy.
Wakati huo huo, taarifa ya Waziri Ummy inaeleza kwamba, wagonjwa wa COVID-19 wameongezeka kutoka 25 hadi kufikia 32, ambapo Tanzania Bara imethibitisha wagonjwa wapya watano na Zanzibar wagonjwa wawili.
Amesema wagonjwa watano kati ya 32 wamepona, na wengine 24 wanaendelea vizuri na matibabu.
Serikali imewataka wananchi kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na maambukizi ya ugonjwa huo.
Leave a comment