TUME ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) nchini Tanzania, imewarejesha wagombea ubunge 19 baada ya kuzifanyia kazi rufaa 22. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma … (endelea).
Pia, Tume hiyo imewarejesha wagombea udiwani 26 wa udiwani na kuzikataa rufaa 19 zilizowasilishwa na walalamikaji.
Huu ni mwendelezo wa NEC kutoa taarifa za uamuzi wa rufaa inazozifanyia kazi ambazo zimewasilishwa na wagombea kupinga uamuzi wa wasimamizi wa ucjaguzi wa majimbo na kata.
Taarifa iliyotolewa leo Alhamisi tarehe 10 Septemba 2020 na Mkurugenzi wa Uchaguzi, Dk. Wilson Mahera imesema tayari imezifanyia kazi rufaa 111 za ubunge na 45 za udiwani.
Itakumbukwa, NEC imewahi kusema jumla ya rufaa zilizowaslishwa ni zaidi ya 500 ambazo zinapaswa kufanyiwa kazi kabla ya Uchaguzi Mkuu utakaofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020.
Kampeni za uchaguzi huo zimekwisha kuanza tangu tarehe 26 Agosti na zitahitishwa 27 Oktoba 2020.
Dk. Mahera amesema, kati ya rufaa hizo 22 za ubunge, imekubali 19 na kuwarejesha katika orodha ya wagombea ubunge na rufaa tatu imezikataa.
Ameyataja majimbo ya wagombea hao kuwa ni; Tunduru Kaskazini, Mbeya Vijijini, Songea Mjini, Karagwe, Ulanga, Chemba, Tanga, Kibamba, Nyasa, Same Mashariki, Buhigwe, Mufindi Kusini, Muheza, Tabora Kaskazini, Ubungo (2) na Kigamboni (3).
Dk. Mahera amezitaja rufaa tatu walizozikataa ni kutoka majimbo ya Kalambo, Kigamboni na Muheza.
Katika awamu ya kwanza iliyotolewa juzi Jumanne, NEC ilitoa uamuzi wa rufaa 55 za ubunge ambapo 15 iliwarejesha wagombea na 40 kati ya hizo ilizozikataa ni 15 waliopinga kutoteuliwa na 25 walikuwa wanapinga wagombea kuteuliwa.
Jana Jumatano, NEC ilitoa taarifa ya rufaa zingine 34 za ubunge kati ya hizo, 13 iliwarejesha kugombea ubunge, 21 ikizikataa.
Soma taarifa yote ya NEC inayohusisha majimbo na kata zilizofanyiwa uamuzi;
Leave a comment