WAZIRI wa Ujenzi, Innocent Bashungwa amesema Serikali inajipanga kutafuta namna ya kuwaondolea adha ya mafuriko wananchi katika barabara ya Mwenge – Bagamoyo jijini Dar es Salaam. Anaripoti Danson Kaijage, Dodoma… (endelea).
Bashungwa ametoa kauli hiyo bungeni jijini Dodoma leo Jumanne wakati akijibu swali la swali la Mbunge wa Urambo, Margaret Sitta (CCM) aliyehoji ni lini Wizara Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi itasafisha mifereji iliyozibwa wakati wa ujenzi wa barabara ya Bagamoyo.
Pia amewaagiza Mameneja wa Mikoa wa Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) mikoa yote nchini kukarabati mifereji iliyo pembezoni mwa barabara kuu ili kuzuia athari zinazoweza kujitokeza wakati wa mvua ikiwemo kuharibika kwa barabara.
“Nitumie nafasi hii niwaelekeze Mameneja wa TANROADS mikoa yote nchini kufika kwenye maeneo ambayo yana changamoto kama wabunge walivyosema na kuona namna ambavyo tunaweza kukakabiliana na jambo hili kwa dharura na haraka,” amesisitiza Bashungwa.
Aidha, katika swali la nyongeza la Mbunge wa Kawe Askofu Josephat Gwajima (CCM) alihoji ni lini ujenzi wa barabara ya Mabasi yaendayo haraka inayoanzia Mwenge – Tegeta – Basihaya itaanza kujengwa.
Akijibu swali hilo Naibu Waziri wa Ujenzi, Mhandisi Godfrey Kasekenya amesema hatua iliyopo kwa sasa ni hatua ya awali kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo na tayari mkandarasi yupo eneo la ujenzi.
“Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hatua iliyopo sasa hivi ni hatua za awali kwa ajili ya kuanza kuijenga barabara hiyo na wakandarasi wapo wanafanya maandalizi ya awali kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo”, amesema Mhandisi Kasekenya.
Leave a comment