TAASISI ya Wajibika, imeanzisha mradi wa Afya Shirikishi mkoani Dodoma, wenye lengo la kuimarisha mifumo ya utoaji na upokeaji huduma za afya kupitia njia ya ushirikishaji. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Mradi huo umeanzishwa mwishoni mwa Aprili 2023, huku mafunzo yake yakiendelea kutolewa kwa baadhi ya watoa na wapokea huduma za afya katika kata nne za Dodoma, ikiwemo Mkonze, Matumbuli, Ihumwa na Chang’ombe.
Akizungumza katika mafunzo kuhusu mradi huo, yaliyotolewa katika Kata ya Mkonze, Mratibu wa Mradi wa Afya Shirikishi, John Mwilongo, ametaja sababu za kuanzisha mradi huo akisema ni kuondoa malalamiko ya wananchi juu ya kutoridhishwa na huduma za afya zitolewazo katika vituo vya afya na hospitali.
“Tuliona kwa nini kunakuwa na malalamiko ya wananchi kwamba nimeenda hospitali huduma haziridhishi, tukaona tuje na mradi huu ili kupunguza manung’uniko hayo,” amesema Mwilongo.
Mwilongo amesema mradi huo una lengo la kuimarisha mifumo ya utoaji na upokeaji huduma za afya, pamoja na kutoa fursa kwa wananchi kujifunza kwa karibu namna vituo vya afya vinavyotoa huduma ili kupunguza manung’uniko yanayoweza kuepukwa.
Mwenyekiti wa Kamati ya Afya Kata ya Mkonze, Shadrack Lucas, amesema mafunzo yanayotolewa kupitia mradi huo yamesaidiwa kuweka uwazi na uwajibikaji katika utoaji huduma za afya kwa kuwa wananchi.
“Kabla hatujapata elimu hii tulikuwa hatujui vitu vingi lakini baada ya semina tuliyopata tumefahamu sisi wanajamii tunatakiwa vitu gani tuvijue na tuvifanyie kazi. Mfano zamani kulikuwa hakuna uwazi wa mapato na matumizi katika vituo vya afya lakini Sasa wameweka baada ya kuhoji,” amesema Lucas.
Baada ya mradi huo kuanza katika Kata ya Mkonze, unatarajiwa kwenda katika Kata nyingine nne zilizopangwa kunufaika na mradi huo.
Leave a comment