KLABU ya soka ya Simba itakosa huduma ya wachezaji wake wanne, ambao wanakabiliwa na majeraha kwenye mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara hii leo tarehe 3 Novemba 2021, dhidi ya na Namungo Fc. Anaripoti kelvin Mwaipungu…(endelea)
Mchezo huo wa duru la tano, utapigwa majira ya saa 1 usiku, kwenye dimba la Benjamin Mkapa, jijini Dar es Salaam.
Wachezaji hao ambao watakosekana kwenye mchezo wa leo ni Chris Mugalu, Ousmane Sakho, Mzamiru Yassin na Thadeo Lwanga ambao wote wanakabiliwa na majeruhi.
Taarifa ya kuwakosa wachezaji hao kwenye mchezo huo wa leo, ilitolewa jana Tarehe 2 Novemba 2021, na kocha msaidizi wa kikosi hiko Seleman matola alipokuwa akizungumza na wanahabari kuelekea mchezo huo wa leo.
“Kwenye mchezo wa kesho (leo) tutawakosa wachezaji wanne ambao ni Mzamiru, Mugalu, Sakho na Lwanga kutokana na kutopona vizuri majerahi yao mara baada ya kuumia.” Alisema Matola
Simba inaingia kwenye mchezo huo wa leo, huku ikiwa na kumbukumbu ya kulazimishwa sare kwenye mchezo uliopita dhidi ya Coastal Union ya kutoka Tanga.
Kwenye msimamo wa Ligi mpaka sasa Simba inapointi nane, kufuatia kupata ushindi katika michezo yake miwili na sare mbili, huku ikiwa kwenye nafasi ya nne.
Katika michezo saba waliokutana kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara, Simba imefanikiwa kuibuka na ushindi mara sita, na matokeo mazuri aliyoyapa Namungo mbele ya Simba ni kupata sare.
Mara baada ya mchezo huo wa leo, Ligi hiyo itasimama kwa wiki mbili kupisha michezo ya kimataifa ya kufuzu fainali za kombe la Dunia.
Leave a comment