RAIS wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Dk. Hussein Alli Mwinyi amesema kuwa kuwa yupo tayari kukaa na wadau wa michezo visiwani humo ili kuangalia mambo ya kujenga katika sekta hiyo ambayo kwa sasa imepoteza mvuto. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Dk. Mwinyi ameongea hayo leo wakati alipokuwa akijibu maswali ya waandishi wa habari muda mfupi mara baaada ya kutangaza baraza lake la mawaziri toka alipoingia madarakani.
Akijibu moja ya swali liliolizwa na mwandishi kuwa ni namna gani atainua sekta ya michezo visiwani humo, Rais Mwinyi alisema kuwa atampa jukumu waziri husika na yupo tayari kukaa na wadau ili waangalie mambo ya kujenga katika sekta hiyo.
“Nipo tayari kukaa na wadau wa michezo ili tuangalie mambo ya kujenga, tufanye na nipo tayari na nitampa jukumu Waziri husika na tukae na wadau ili michezo irudi katika hadhi yake kama siku za nyuma,” alisema Dk. Mwinyi.
Tayari Rais Hussein Alli Mwinyi amemteua Tabia Mwita Maulid kuwa Waziri wa Vijana, Utamaduni Sanaa na Michezo ambaye atakwenda kuanza majukumu hayo mapya mara baada ya kuapishwa Jumamosi tarehe 21 Novemba, 2020 saa 5:00 asubuhi.
Siku za hivi karibuni michezo kwenye visiwani humo imeshuka na kupelekea Ligi Kuu Zanzibar kuchezwa kwa misimu mitatu bila kuwa na mdhamini hivyo kupunguza ubora wa ligi na klabu shiriki.
Leave a comment