WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Prof. Joyce Ndalichako amewataka waajiri wote nchini kuchukua hatua ya kuhakikisha wanalinda usalama na afya za wafanyakazi wao kama yalivyomatakwa ya Sheria ya Afya na Usalama Mahali pa Kazi Namba 5 ya mwaka 2003. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro … (endelea).
Pia amewaagiza kushirikiana na Wakala wa Afya na Usalama mahali pa kazi (OSHA) kuwapatia wafanyakazi elimu ya namna ya kutumia mifumo itakayostawisha mazingira ya afya na usalama mahali pa kazi.
Prof. Ndalichako ametoa kauli hiyo leo tarehe 28 Aprili 2023 mjini Morogoro katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi ambayo kitaifa yamefanyika katika viwanja vya Tumbaku mkoani humo.
Mwaka huu maadhimisho hayo yaliyoanza tarehe 26 na kutarajiwa kuhitimishwa tarehe 30 Aprili mwaka huu, yamebeba kaulimbiu inayosema “Mazingira Salama na Afya ni Kanuni na Haki ya Msingi Mahali pa Kazi.”
Amesema ili kuzuia magonjwa, ajali na vifo katika maeneo ya kazi, wajiri wanatakiwa kuweka mifumo sahihi ya usalama na afya sehemu za kazi.
“Mifumo hiyo izingatie vihatarishi… kama ni sehemu za ukataji vyuma, uzalishaji kwa ujumla kila eneo la kazi linakuwa na viatarishi vyake hivyo ili lisiathiri utendaji ni vema kuweka mifumo dhabiti,” amesema.
Amesema iwapo waajiri watalegalega kuweka mifumo hiyo, utendaji kazi wale wanaoumia au wanapopata matibabu utapungua.
Akitoa salamu za waajiri, Afisa Mtendaji Mkuu wa Chama cha Waajiri (ATE), Suzanne Ndomba-Doran amesema ikiwa ATE ndiyo sauti ya waajiri wote nchini kwa kushirikiana na wadau imekua mstari wa mbele kuwahimiza waajiri kuzingatia na kutekeleza matakwa ya Sheria ya Afya na Usalama mahala pa kazi ya mwaka 2003.
Amesema sheria hiyo inamtaka mwajiri kutengeneza mazingira yenye afya na usalama mahali pa kazi.
Pia ametoa rai kwa wafanyakazi kufuata kanuni na taratibu zilizowekwa mahala pa kazi ili kuepusha migogoro isiyo ya lazima inayoweza kushusha kwa ufanisi katika maeneo ya kazi.
Naye Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Afya na Usalama mahali pa kazi (OSHA), Khadija Mwenda amesema siku ya usalama na afya duniani ni siku muhimu ya kimataifa ambayo nchi zote wanachama wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) zilianza kuadhimisha siku kuanzia mwaka 2003.
Amesema lengo la maadhimisho hayo ni kuwawezesha wadau kupanua uelewa kuhusu ukubwa na madhara ya ajali na magojwa yatokanayo na kazi na kujenga uwezo katika kuweka sera na mikati ya kuzuia ajali na magonjwa kazini ili kufanya kazi zote ziwe za staha.
Maadhimisho haya yamehudhuriwa pia na Viongozi mbalimbali akiwemo Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Prof. Jamal Katindu; Jaji Mfawidhi, Mahakama Kuu ya Tanzania -Divisheni ya Kazi, Dk. Yose Joseph Mlyambina; Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ustawi na maendeleo ya jamii, Fatma Hassan Tawfiq; Mwakilishi wa Shirika la Kazi Duniani, Getrude Sima; Viongozi wa Shirikisho la Vyama vya Waajiri nchini wakiongozwa na Rais wake, Tumaini Nyamhokya pamoja na viongozi mbalimbali na wakuu wa taasisi binafsi na umma.
Pamoja na mambo mengine maadhimisho haya pia yameenda sambambamba na tukio la utoaji wa tuzo kwa waajiri waliofanya vizuri katika eneo la afya na usalama.
Leave a comment