WAZIRI wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nauye amewataka Watanzania kutumia vizuri mawasiliano kujiajiri na kujiletea maendeleo badala ya kutapeli watu. Anaripoti Walter Mguluchuma, Katavi … (endelea).
Nape ametoa wito huo leo tarehe 10 Januari, 2023 wilayani Mlele mkoani Katavi wakati akizindua mnara wa mawasiliano uliojengwa na TTCL kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Amesema Watanzania watumie uwepo wa mawasiliano hayo kujipatia ajira na si kudanganya watoto wadogo, na wanafunzi wa kike.
Nape amesisitiza kuwa wananchi watumie mawasiliano hayo kwa ajili ya maendeleo ya kilimo na biashara mbambali zitakazoweza wapatia fedha.
Amesema miradi hiyo ya minara imejengwa kwa fedha za walipa kodi hivyo ni mali ya wananchi wenyewe ambao pia wanajukumu la kuilinda na kuitunza.
Aidha, amesema Serikali inajua simu za kisasa gharama zake ni kubwa hivyo imeanza mazungumzo na watoa huduma mbalimbali wa mitandao waanzishe utaratibu kwa watu kupata simu za kisasa hata kwa mkopo na mazungumzo yanakwenda vizuri.
Mtendaji Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa wote, Justina Mashiba amesema mamlaka hiyo inatekeleza shughuli zake kwa kuwa na miradi nchi nzima kwenye kila wilaya na mikoa.
“Mpaka sasa wameshirikiana na watoa huduma mbambali wa mawasiliano kama TTCL, Tigo, Vodacom, Airtel na makampuni mengine wameshasaini mikataba ya ujenzi wa minara 1,242 ya mawasiliano kwa nchi nzima na kati ya minara hiyo minara 1,087 imeshakamilika.
Amesema minara 155 iliyobaki ipo kwenye hatua mbambali za ukamilishwaji na itakapokuwa imekamilika na kufikia minara 1242 watakuwa wamewafikia Wanzania milioni 15.
Naye Mkurugenzi Mkuu wa TTCL, Peter Ulanga amesema Shirika hilo linaendelea kuboresha mawasiliano kwenye maeneo yote ambayo hayana mawasiliano yakiwepo maeneo ya mikoa ya pembezoni.
Leave a comment