SERIKALI imepiga marufuku huduma ya bweni kwa wanafunzi wa umri mdogo kuanzia darasa la awali hadi darasa la nne. Anaripoti Judith Mbasha, DSJ … (endelea).
Agizo hilo limetolewa tarehe 28 Februari 2023 na Kamishna wa Elimu, Dk. Lyabwene Mtahabwa, kupitia Waraka wa Elimu Na. 2 wa mwaka 2023 unaohusu huduma ya kulaza wanafunzi bweni kwa ngazi ya awali na shule za msingi.
Katika waraka huo Dk. Mtahabwa amesema waraka huo utaanza kutekelezwa rasmi tarehe 1 Machi, 2023 ambapo huduma ya bweni zitaendelea kutolewa kuanzia darasa la tano na kuendelea.
Dk. Mtahabwa amesema agizo hilo la serikali linaakisi utekelezaji wa waraka wa elimu Na.3 wa mwaka 2007, unaohusu kukataza kambi za masomo katika shule za msingi.
Miongoni mwa sababu zilizosababisha marufuku hiyo, Dk. Mtahabwa amesema ni kubainika kwa makambi mengi kuwa na mazingira hatarishi kimaadili, usalama na afya za wanafunzi kutokana na kuanzishwa bila kufuata utaratibu rasmi za unzishwaji bweni au makazi ya pamoja ya wanafunzi.
Aidha ametaja sababu zingine kuwa ni kulingana na tafiti zilizopo kuonesha madhara ya muda mrefu yotokanayo na kulaza bweni watoto wenye umri mdogo.
Amesema kwa mujibu tafiti hizo kitendo hicho kinapelekea watoto hao kukosa mapenzi na upendo wa dhati kutoka kwa wazazi na walezi wao, pia hata kukosa ushirikiano mzuri katika jamii zinazo wazunguka.
Pia ametoa msisitizo juu ya agizo kutekelezwa ipasavyo kwani kutakuwa na ufatiliaji wa mara kwa mara ili kubaini shule ambazo zitaenda kinyume na agizo hilo na kwamba hatua za kinidhamu na kisheria zitachukuliwa ikiwemo kufutiwa usajili.
Sambamba na hayo serikali imewataka wamiliki wote wa shule nchini kuwa na kibali maalum kutoka kwa Kamishna wa Elimu endapo kutakua na ulazima au sababu muhimu za kuanzishwa huduma za bweni katika ngazi hiyo.
Leave a comment