Mwanaume mmoja ambaye hajafahamika jina lake ameuawa na wananchi wenye hasira kali baada ya kujaribu kuiba katika duka moja lililopo kwenye Soko la Ngeze lililopo Kijiji cha Igale Kata ya Iyula wilayani Mbozi mkoani Songwe. Anaripoti Ibrahim Yassin… Songwe (endelea).
Akizungumza na MwanaHALISI Online leo Jumamosi kwa njia ya simu Diwani wa Kata ya Iyula, Charles Shonza amesema mtu huyo ameshambuliwa usiku wa kuamkia leo baada ya mlinzi wa soko hilo kuita watu kwa ajili ya kumsaidia kumkamata mhalifu huyo.
Shonza ameeleza kuwa katika tukio hilo la wizi huo lilihusisha watuhumiwa watatu ambapo wengine wawili wamekimbia na mpaka sasa hawajulikani walikotokea.
Naye Kaimu Mwenyekiti wa Kijiji cha Igale, Jelih Siwale amesema watu hao wamebomoa duka la mfanyabiashara Hassan Ndaga na kuharibu mashine ya kuchezeshea bahati na sibu kisha kuchukua fedha zilizokuwa ndani yake.
Aidha, Siwale amesema Jeshi la Polisi kata ya Iyula limefika eneo la tukio na uchunguzi unaendelea.
Kamanda wa polisi mkoani Songwe, Augustino Senga amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kuongeza kuwa tayari taratibu za kipolisi zimefanyika.
Amesema jeshi hilo linalaani wananchi kujichukulia sheria mkononi na kwamba waliohusika kumuua mtuhumiwa watakamatwa na kushtakiwa kwa kufanya mauaji.
Amesema jeshi hilo lipo kwa ajili ya kukamata wahalifu na Mahakama zipo kwa ajili ya kutoa haki na hukumu hivyo ni lazima watu wafuate sheria na si kujichukulia sheria mkononi.
Leave a comment