RAIS John Magufuli amewataka Watanzania kuwaombea mawaziri, akisema kwamba wanafanyakazi kwa mateso makubwa. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Rais Magufuli ametoa wito huo leo tarehe 5 Oktoba 2019, akizungumza na wananchi kwenye ziara yake mkoani Songwe.
Rais Magufuli ameeleza kuwa, katika uongozi wake mawaziri hawafaidiki kiasi kwamba watu wanawaonea huruma.
Mkuu huyo wa nchi amesema, sio kwamba hawapendi mawaziri wake bali analazimika kufanya hivyo. Na kuwa, mawaziri wake hawana uhakika na kesho yao, kama wataendelea kuwa mawaziri.
“Katika kipindi ambacho mawaziri hawakufaidika ni wakati wnagu. Kwanza, hata wanapolala hajui hata kama kesho ataamka akiwa waziri. Najua watu wanawaonea huruma, laikini lazima nifanye hivyo. Sio kwamba siwapendi, wanafanya kazi kwa mateso makubwa na wao muwaombee sana,” amesema Rais Magufuli.
Wakati huo huo, Rais Magufuli amesema hawezi akaondoka madarakani huku akiwaacha Watanzania hawana maendeleo.
“Unajiuliza vituo hivi (vya afya) 352 vimekamilika kujengwa, tumeokoa roho za watanzania wangapi masikini? Kweli niondoke niwaache hawa kwa sababu tu ya unafiki wangu, kwamba natakiwa niondoke nimechoka?
Hapo ndipo ninapopata nguvu ya kusema lazima niendelee kufanya kazi, na ndio maana ninawaomba sana wana Songwe na wenzangu muendelee kuniombea na kuwaambea viongozi wenzangu mawaziri wanafanya kazi sana,” amesema Rais Magufuli.
Rais Magufuli amesema hana imani kama akiondoka madarakani, miradi anayoitekeleza, kama itafanyiwa kazi na watakaokuja baada yake.
“Lakini saa nyingine ukishajiuliza mateso ya watu ambao wanayapata, inakubidi useme lazima mimi nifanye. Ilikua ni lazima nifanye mimi. Ukiangalia namna ukiicha nchi, je hii miradi kweli itatekelezwa, je nikiondoka leo Stiglers Gorge ijtajengwa?, nikiondoka leo Standard Gauge itajengwa?” amehoji Rais Magufuli na kuongeza;
“Je, nikiondoka leo ndege zitanunuliwa? Mbona hazikununuliwa miaka yorte? Hapo ndipo ninapojisikia, ninasema lazima nifanye kazi.”
Leave a comment