DAKTARI Mwele Malecela, Mkurugenzi wa Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa Afrika vya Shirika la Afya Duniani (WHO), amesema ‘hatumiki’. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Jana tarehe 4 Oktoba 2019, kupitia ukurasa wake wa twitter, Dk. Mwele amesema iko siku, watu wataujua ukweli kuhusu madai ya ugonjwa wa ZIKA.
Dk. Mwele alisema hayo kutokana na kushambuliwa kwa matusi na baadhi ya watu, tukio lililotokea saa kadhaa baada ya Rais John Magufuli kumtuhumu kwamba, alitumiwa kuichafua nchi.
Dk. Mwele amesema, watu hao wanaomtukana na kumkebehi, hawaufahamu ukweli, na kwamba ipo siku wataufahamu.
“Kuna watu mmevamia TL yangu na matusi na kebehi, hamjui ukweli na badala ya kuuliza mnafyatua matusi. Iko siku mtaujua ukweli,” Dk. Mwele ameandika kwenye ukurasa wake wa twitter.
Malalamiko ya Dk. Mwele kutukanwa, yamekuja kufuatia madai ya Rais Magufuli, kwamba kuna mtendaji wake ambaye hakumtaja jina, alitumwa kutangaza kuwa Tanzania kuna virusi vya Zika, ili kuzuia watalii wasije nchini.
Rais Magufuli alieleza zaidi kuwa, baada ya mtendaji huyo kutangaza uwepo wa Zika alimfukuza kazi, na kisha kupewa kazi na watu waliomtuma kuutangaza ugonjwa huo.
“Kuna mtendaji wangu alitangaza kuwa kuna virusi vya Zika nchini Tanzania, nikamfukuza usiku saa saba. Sikutaka kumchelewesha, nilivyomfukuza tu wakampa kazi huko akawa bosi kumbe walimtuma kutangaza kuwa tuna ugonjwa huo ili watalii wasije nchini kwetu,” alisema Rais Magufuli.
Rais Magufuli alimuondoa Dk. Mwele kwenye wadhifa wa Ukurugenzi wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR), siku moja baada ya kutoa ripoti ya utafiti wa magonjwa.
Ripoti hiyo ilidai kwamba, Mikoa ya Morogoro, Geita na Magharibi wa Tanzania kuna virusi vya ugonjwa wa Zika.
Baada ya kuondolewa NIMR, Dk. Mwele aliteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Mpango Maalumu wa WHO wa kutokomeza magonjwa yasiyopewa kipaumbele (ESPEN).
Leave a comment