MTANDAO wa Watetezi wa Haki za Binadamu Tanzania (THRDC), umemshauri Rais Samia Suluhu Hassan, aunde tume ya kudumu ya kitaifa, kwa ajili ya uchunguzi wa matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu, ikiwemo mauaji yanayodaiwa kufanywa na maafisa wa vyombo vya dola. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Ushauri huo ulitolewa jana Jumamosi, tarehe 4 Februari 2022 na Mratibu wa THRDC, Onesmo Olengurumwa, baada ya Rais Samia kumwagiza Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa kuunda kamati maalumu ya kuchunguza mauaji yaliyotokea hivi karibuni mkoani Mtwara.
Matukio hayo ni mauaji ya mfanyabiashara wa madini mkoani Mtwara, Mussa Hamisi na mauaji ya watu yaliyotokea katika mapigano baina ya wakulima na wafugaji, Kilindi mkoani Tanga.
“Ukweli ni kwamba, Tanzania haina tume ya kudumu ya kopokea na kuchunguza tuhuma dhidi ya vyombo vya usalama. THRDC inatumia fursa hii kumshauri Rais Samia kuanzisha tume maalum na ya kudumu, itakayohusika na kufuatilia na kufanya uchunguzi kuhusu ukiukwaji wa haki za binadamu katika idara za serikali na vyombo vya usalama,” amesema Olengurumwa.
Mratibu huyo wa THRDC amesema kuwa, uwepo wa tume ya kudumu ya uchunguzi wa matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu, utasaidia haki kuoatikana kwenye tuhuma wananchi wanazoelekeza katika vyombo vya usalama.
“Misingi ya utoaji haki hukataza mtuhumiwa asiwe mchunguzi wa shauri linalo mhusu, pamoja na pongezi hizi tunashauri kamati hizi ziwe zinaundwa kwa uwakilishi toka sekta mbalimbali ikiwemo
wawakilishi kutoka sekta binafsi, mahakama au watetezi wa haki, Asasi za Kiraia, yatakayosaidia katika kupatikana kwa haki,” amesema Olengurumwa.
Aidha, mtandao huo umeipongeza hatua ya Rais Samia kuagiza uundwaji wa kamati hiyo, kwa kuwa imedhihirisha kwamba ana dhamira ya kulinda haki za Watanzania.
Tayari Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameunda timu ya watu tisa kwa ajili ya uchunguzi wa mauaji hayo, yenye wajumbe kutoka mamlaka za Serikali, ikiwemo Ofisi ya Taufa ya Mashtaka, Ofisi ya Rais, Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Timu hiyo imepewa siku 14 kuanzia leo Jumamosi.
Leave a comment