SERIKALI Visiwani Zanzibar, imeanza uchunguzi wa chanzo cha vifo vya kaa chanje, walioonekana katika fukwe mbalimbali zilizopo katika kisiwa cha Unguja. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Kaa hao walianza kuonekana Septemba 28, akitapakaa kwenye fukwe mbalimbali, ikiwamo Mtoni, Mzingani, Kilimani, Ngazimia na Forodhani.
Taarifa za awali zinaonyesha kuwa mabadiliko ya tabia nchi yameleta athari hizo na kwamba kuna mabadiliko katika maji ya bahari yanayotokana na mawimbi yaliyosababisha kaa hao kufa.
Mkurugenzi wa Maendeleo na uvuvi wa Zanzibar, Dk. Salum Soud, amenukuliwa akisema, serikali inaendelea na uchunguzi wa kina kufahamu haswa nini chanzo cha vifo hivyo.
Hata hivyo, Dk. Soud bado anasisitiza kuwa “mabadiliko ya hali ya hewa ni moja ya sababisho la vifo hivyo.”
Dk. Soud, ambaye ni mwanasayansi na mtaalamu wa masuala ya majini, alisema kuwa Kaa hao walishuhudiwa wengi 20 na 28 Septemba, na si kwa wingi kati ya tarehe 2, 10 na 11 Oktoba 2022.
Alisema, “sasa tunachunguza chanzo, lakini baadhi ya viumbe hai kama kaa nyakati nyingine hushindwa kustahimili mabadiliko ya ghafla baharini, na hivyo kusababisha kufa.
“…maji ya bahari yana tabaka la joto na baridi, jambo ambalo linasababisha mawimbi na kuyalazimisha maji chini kwenda juu.
“Kitendo hicho, husababisha oksijeni kupungua kwa hivyo kaa wanaweza kukabiliwa na vifo,” alieleza.
Amewataka wananchi wa kawaida, wavuvi na watalii, kutokuwa na wasiwasi kwa kuwa kilichopo hakihusiani na uchafuzi wa mazingira.
Leave a comment