WIZARA ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, imeagiza taasisi za umma na watu binafsi zaidi 200 zinazodaiwa kodi ya pango la ardhi na malimbikizo ya muda mrefu, kuhudhuria kikao maalum kitachofanyika tarehe 11 Juni 2019, jijini Dodoma. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa tarehe 5 Juni 2019 na Dorothy Mwanyika, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, taasisi hizo zitakaposhindwa kufika katika kikao hicho, hatua za kufuta milki zao na kuuza viwanja husika zitafuata kwa mujibu wa sheria.
Taarifa hiyo imeeleza kuwa, mashirika, taasisi na makampuni yanayodaiwa kodi ya pango la ardhi yanatakiwa kufika na nyaraka za umiliki pamoja na stakabadhi za malipo yote yaliyofanyika, katika kikao hicho baina yao na Waziri wa Wizara hiyo, William Lukuvi.
Aidha, taarifa hiyo imetoa wito kwa wadaiwa hao kwenda kulipia madeni yao kwa hiari, katika ofisi za ardhi zilizoko karibu na maeneo yao, kwa kuwa ofisi hizo ziko wazi siku zote.
Miongoni mwa taasisi hizo ni pamoja na Exim Bank Tanzania Limited, Efatha Ministry, Dar es Maritime Institute, CRDB Bank PLC, College Business Education, Chuo cha Ushirika Moshi (MUCCOB), Bodi ya Korosho Tanzania.
Leave a comment